Ziara Rasmi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchini Urusi imeendelea kuzaa matunda katika sekta ya elimu, baada ya wanafunzi 10 waliofanya vizuri katika masomo ya sayansi kupata ufadhili wa masomo katika Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi (RUDN University) kilichopo jijini Moscow.
Wanafunzi hao waliomaliza kidato cha sita na kufanya vizuri katika tahasusi za PCM, PGM na PMC, wamepata fursa hiyo kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended, ikiwa ni sehemu ya matokeo ya ziara ya Rais Samia nchini Urusi iliyofanyika mwezi Juni 2026.
Rais Samia alifanya ziara hiyo nchini Urusi na kutunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) na RUDN University, moja ya vyuo vikuu vinavyotambulika nchini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Agosti 13, 2026, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda, amesema wanafunzi hao wamechaguliwa kutokana na kufanya vizuri kitaaluma, wakifuata kundi la wanafunzi 50 waliokuwa wamechaguliwa awali.
Prof. Mkenda amesema wanafunzi hao 10 wamechaguliwa kuanzia nafasi ya 51 hadi ya 60, ambapo wanafunzi saba wametoka katika shule za Serikali na watatu kutoka shule za binafsi.
“Wanafunzi hao wanatarajiwa kufanya kambi ya mafunzo nchini Urusi kwa takribani miezi 10. Serikali ya Urusi itagharamia mafunzo hayo kwa asilimia 80, huku Serikali ya Tanzania ikigharamia asilimia 20. Watakapoanza mafunzo ya chuo kikuu mwezi Septemba 2027, Serikali ya Urusi itagharamia kwa asilimia 100,” amesema Prof. Mkenda.
Kwa upande wa wanafunzi 50 waliopata ufadhili katika awamu ya kwanza, Waziri Mkenda amesema wote wamekubali fursa hiyo ya kusoma nje ya nchi na wanatarajiwa kuanza kambi ya mafunzo Septemba 14, 2026.
Amesema kambi hiyo itafanyika kwa muda usiozidi miezi 10 katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST), Arusha, kabla ya wanafunzi hao kuanza masomo katika vyuo vya nje ya nchi.
Waziri Mkenda amesisitiza kuwa fursa hizo za ufadhili ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuwawezesha vijana wa Kitanzania kupata elimu bora na kuongeza ujuzi utakaochangia katika maendeleo ya Taifa.
Aidha, amewataka wanafunzi wanaopata fursa za kusoma nje ya nchi kutumia nafasi hizo kwa kufanya vizuri katika masomo yao, akieleza kuwa mafanikio yao yanaweza kuongeza imani na ushawishi kwa nchi wahisani kuendelea kutoa nafasi zaidi za ufadhili kwa Watanzania.
Amesema kufanya vizuri kwa wanafunzi hao kutasaidia Tanzania kupata fursa zaidi za ufadhili kutoka nchi mbalimbali, hatua ambayo kwa upande mwingine itawezesha rasilimali zilizopo katika mikopo ya elimu ya juu kuwafikia wanafunzi wengi zaidi wanaosoma ndani ya nchi.
Hatua hiyo inaendelea kuonesha namna diplomasia ya Rais Samia inavyoweza kufungua fursa za elimu, ujuzi na maendeleo kwa vijana wa Kitanzania.




Comments
Post a Comment