Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itakamilisha mchakato wa kuunda Halmashauri ya Mwibara ili kusogeza huduma za Serikali karibu na wananchi na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za kijamii na maendeleo. Ametoa kauli hiyo leo Julai 4, 2026, alipohutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Halmashauri ya Mji wa Bunda mkoani Mara, baada ya Mbunge wa Bunda Vijijini, Mhe. Boniface Mwita Getere, kuwasilisha ombi la wananchi la kuanzishwa kwa halmashauri hiyo. Waziri Mkuu alisema Serikali imepokea hoja hiyo na kutambua umuhimu wake, akibainisha kuwa utaratibu wa kuanzisha halmashauri mpya utaendelea kufuatwa ili kuhakikisha huduma za Serikali zinawafikia wananchi kwa ufanisi zaidi. "Nimeipokea hoja hii. Serikali ina utaratibu unaofuatwa katika kugawa maeneo ya kiutawala. Nimemuelekeza Mkuu wa Mkoa pamoja na Sekretarieti ya Mkoa kuendelea na mchakato huo ili Serikali iweze kupeleka mapendekezo kwenye mamlaka husika kwa hatua zinazostahili," alisema Waziri Mkuu. ...
Marato tv - Sauti ya Jamii