WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameendesha harambee na kuchangisha sh. milioni 928.67 za ujenzi wa kanisa kuu tarajiwa la Mt. Andrea Kagwa la Jimbo Katoliki la Lindi. Kati ya fedha hizo, sh. milioni 464.3 ni fedha taslimu na nyingine kati ya hizo zimeshawekwa benki na sh. milioni 464.37 bado ni ahadi. Awamu ya kwanza ya ujenzi huo, inatarajiwa kugharimu sh. milioni 700. Akizungumza na waumini na wadau mbalimbali waliohudhuria harambee iliyofanyika Ruangwa mjini, leo mchana (Jumamosi, Julai 27, 2024), Waziri Mkuu amewataka waliotoa ahadi wazikamilishe mapema ili kazi ya ujenzi isikwame. "Ninawashukuru sana wote mliofika na wote waliochangia ujenzi wa kanisa tarajiwa. Ninawaomba walioahidi, wakamilishe ahadi zao mapema ili kazi ianze kwani ramani ipo, mafundi wapo tayari, wasimamizi wa ujenzi wapo," amesisitiza. Waziri Mkuu amesema uamuzi wa Baba Askofu wa Jimbo Katoliki la Lindi, Mhashamu Askofu Wolfgang Pisa kuanza ujenzi wa kanisa kuu la jimbo hilo, ni utekelezaji ...