Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, leo Agosti 7, 2026, akiwa mgeni rasmi wa zamu, ametembelea mabanda mbalimbali katika Maonesho ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi (Nanenane) yanayoendelea katika Viwanja vya Themi-Njiro, jijini Arusha. Katika ziara hiyo, Mhe. Sendiga ametoa wito kwa wananchi wa mikoa ya Kanda ya Kaskazini kujitokeza kwa wingi kutembelea maonesho hayo ili kujifunza teknolojia mbalimbali za kisasa za kilimo, mifugo na uvuvi zitakazochochea ongezeko la uzalishaji na maendeleo ya kiuchumi. Amesema maonesho hayo yamekusanya wafanyabiashara, wabunifu na wajasiriamali kutoka ndani na nje ya nchi, jambo linalotoa fursa kwa wananchi kupata maarifa, kujifunza ubunifu na kuanzisha ushirikiano wa kibiashara. Maonesho ya Nanenane ya mwaka 2026 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo: "Tambua Soko, Ongeza Tija kwa Kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050."
Dar es Salaam, Agosti 7, 2026 Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekutana na ujumbe kutoka African Leadership Initiative for Impact (ALI) kwa lengo la kujadili fursa za ushirikiano katika maandalizi ya Jukwaa la Amani kwa Vijana, linalotarajiwa kufanyika mwezi Septemba 2026 jijini Dar es Salaam. Majadiliano hayo yalilenga kubaini namna pande hizo mbili zitakavyoshirikiana katika kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika kujenga amani, kukuza uongozi wenye maadili na kuimarisha mshikamano wa kijamii kupitia Elimu ya Uraia wa Dunia (Global Citizenship Education - GCED), ambayo ni moja ya maeneo ya kipaumbele ya UNESCO katika kujenga jamii zenye amani, uvumilivu na maendeleo endelevu. Akizungumza wakati wa kikao hicho, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Profesa Hamisi Malebo, alisema Tume imepokea kwa furaha wazo hilo na kuliona kuwa linaendana na dhamira ya UNESCO ya kujenga amani katika fikra za watu kupitia elimu, sayansi, utamaduni, ma...