Naibu Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mheshimiwa Dkt. Doto Mashaka Biteko amesema kuwa mashindano ya ngalawa race ni miongoni mwa matukio makubwa ya kiburudani yanayoipamba Kizimkazi Festival 2026. Mashindano hayo yamefanyika Kizimkazi, Kusini Unguja Agosti 12, 2026 yaliyokuwa na ushindani mkubwa ambapo Nassor Pandu wa Mkunguni ameibuka mshindi wa mashindano ya ngalawa ikiwa ni sehemu ya shughuli mbalimbali zinazoendelea katika Tamasha la Kizimkazi. “ Ni dhahiri kwamba mashindano haya yamekuwa muhimu kwa vijana na jamii kwa ujumla. Tukio hili limewaleta pamoja wadau mbalimbali na kuchangia kwa kiasi kikubwa juhudi za kuboresha mazingira ya michezo na burudani,” amesema Dkt. Biteko. Dkt. Biteko ameongeza kuwa mashindano ya Ngalawa race Kizimkazi Festival yameendelea kutoa fursa za kiuchumi kwa vijana mbalimbali katika kushindana hadi kupata timu mbili bora za Mchangamle na Mkunguni ambapo kila timu imehusisha manahodha 10.
NA: MWANDISHI WETU, TANGA Katika kuhakikisha wafanyabiashara wanakuwa na uelewa wa kutosha kuhusiana na mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka 2026/2027, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Tanga, imetoa mafunzo kwa wafanyabiashara mkoani humo. Mafunzo hayo yametolewa Agosti 12, 2026, katika Ukumbi wa YDCP Jijini Tanga. Katika mafunzo hayo, wafanyabiashara wamejengewa uwezo juu ya mabadiliko mbalimbali ya sheria za kodi yaliyofanyika ili kuiwezesha TRA kutekeleza majukumu waliyopangiwa na serikali kuu. Akifungua mafunzo hayo, Meneja wa TRA mkoa wa Tanga, CPA. Castro John, amesema sheria zaidi ya 15 za kodi zimefanyiwa mabadiliko, hivyo wanalo jukumu la kutoa elimu kwa wafanyabiashara. "Niwashukuru wafanyabiashara wa Tanga kwa kujitokeza kupata elimu hii muhimu kwani wafanyabiashara wanapokuwa na uelewa wa mabadiliko haya, basi utekelezaji wa ulipaji kodi utakuwa mwepesi," amesema CPA John. Maofisa mbalimbali kutoka TRA Makao Makuu waliwaelimisha wafanyabiashara hao maba...