NA MASHAKA MHANDO, Korogwe WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amemwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga (RPC), ACP Almachius Mchunguzi, kumsaka na kumkamata mkandarasi aliyekimbia baada ya kulipwa Shilingi Milioni 934 kwa ajili ya ukarabati wa mradi wa maji katika mji wa Mombo, wilayani Korogwe. Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo Leo February 14 mara baada ya kukagua mradi wa maji wa Miji 28 unaotekelezwa katika wilaya nne za mkoa wa Tanga, ambapo ameeleza kukerwa na mkandarasi huyo aliyepokea fedha za umma na kutoweka bila kutekeleza mradi, huku wananchi wakiendelea kutaabika na ukosefu wa maji. "Ameondoka na fedha wakati wananchi wanapata shida; haya ndiyo mambo yanayokera na kuchukiza. RPC, huyu mtu atafutwe popote alipo, akamatwe na awekwe ndani mpaka arejeshe fedha za umma. Sijateuliwa ili nipendwe, na sitakuwa na huruma na watu wanaohujumu miradi ya Serikali," alisisitiza Waziri Mkuu. Mradi wa Miji 28 Kufikia Asilimia 75 Mapema, Wazi...