WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amezitaka Kamati za Ushauri wa Stadi (Training Advisory Committees–TACs) za Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuwa chachu ya kuhakikisha mafunzo yanayotolewa yanaendana na mahitaji halisi ya soko la ajira na uzalishaji nchini.
Prof. Mkenda amesema kamati hizo zinapaswa kuwa kiungo madhubuti kati ya VETA, Serikali, waajiri na sekta binafsi, ili kuhakikisha vijana wanaohitimu wanakuwa na ujuzi, umahiri, ubunifu na uwezo wa kutumia teknolojia unaohitajika katika maeneo ya kazi.
Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof Adolf Mkenda Ameyasema hayo leo, Agosti 13, 2026, jijini Dodoma, wakati akizindua rasmi Kamati za Ushauri wa Stadi za VETA, ambapo amesisitiza kuwa mfumo wa mafunzo ya ufundi stadi haupaswi kuishia katika kutoa vyeti pekee, bali unapaswa kuwaandaa wahitimu kwa ajira, kujiajiri na kuanzisha shughuli za uzalishaji.
“Hatupaswi kuwa na mfumo wa mafunzo unaoishia katika kutoa vyeti pekee. Tunataka kuwa na mfumo unaozalisha watu wenye ujuzi, umahiri, ubunifu, nidhamu ya kazi na uwezo wa kutumia teknolojia katika kuongeza tija na ushindani,” amesema Prof. Mkenda.
Amesema wajumbe wa TACs wana nafasi ya kipekee kwa kuwa wako karibu na mabadiliko ya teknolojia, uzalishaji na mahitaji ya waajiri, hivyo wanapaswa kuishauri VETA kwa wakati kuhusu stadi mpya zinazohitajika na mabadiliko yanayopaswa kufanyika katika mitaala.
Prof. Mkenda amewataka wajumbe hao kutokuwa kamati za mikutano pekee, bali kuwa “Kamati za Matokeo” kwa kubaini mapema mabadiliko katika sekta mbalimbali na kutoa ushauri unaoweza kusaidia VETA kuboresha programu za mafunzo.
Amesema ushauri wa kamati hizo unaweza kuamua iwapo kijana anayehitimu atakuwa na ujuzi unaohitajika katika eneo la kazi au kubaki na cheti kisichokidhi mahitaji ya mwajiri.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, maeneo yenye fursa kubwa ambayo yanahitaji kupewa kipaumbele katika mafunzo ni pamoja na ukarimu, utalii, sanaa, TEHAMA, uzalishaji, ujenzi, nishati na kilimo.
Prof. Mkenda amesema kuanzishwa kwa TACs kunakuja wakati Tanzania ikiwa katika hatua muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inaweka mkazo katika kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani pamoja na kuongeza uwezo wa watu na maendeleo ya jamii.
Amesema utekelezaji wa Dira hiyo hauwezi kufanikiwa bila kuwa na nguvu kazi yenye maarifa, ujuzi na uwezo wa kutumia teknolojia na ubunifu.
“Hatuwezi kuwa na uchumi imara, jumuishi na shindani bila kuwa na watu wenye ujuzi. Hatuwezi kujenga viwanda vya kisasa bila kuwa na mafundi, mafundi sanifu, wataalamu wa teknolojia na watu wenye uwezo wa kuendesha na kutengeneza mifumo ya kisasa,” amesema.
Aidha, amesema Tanzania haiwezi kujenga uchumi wa kidijitali bila vijana wenye ujuzi wa TEHAMA, huku akisisitiza umuhimu wa kuwa na uwezo wa kuzalisha bidhaa na huduma kwa kutumia maarifa, teknolojia na ubunifu wa ndani.
Waajiri watakiwa kushiriki katika mafunzo
Prof. Mkenda amewataka waajiri na sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika mfumo wa mafunzo ya ufundi stadi kwa kueleza aina ya ujuzi, teknolojia, vifaa na viwango vya utendaji vinavyohitajika katika maeneo ya kazi.
Amesema Serikali imedhamiria kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu na sekta ya viwanda kupitia Mpango wa Kitaifa wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Sekta ya Viwanda katika Ukuzaji wa Ujuzi na Uwezeshaji wa Ajira, uliozinduliwa Februari 9, 2026, jijini Dar es Salaam.
Amesema mpango huo unalenga kuoanisha mafunzo na mahitaji halisi ya soko la ajira pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu na sekta ya uzalishaji.
Kwa upande mwingine, amewataka wajumbe wa TACs kuwa mabalozi wa VETA katika sekta wanazotoka kwa kuwahamasisha waajiri kushirikiana na taasisi hiyo katika kuandaa mitaala, kutoa mafunzo kwa vitendo, kuboresha teknolojia na kuandaa nguvu kazi yenye ujuzi unaohitajika.
Prof. Mkenda amesema mafunzo ya ufundi stadi yanapaswa pia kutoa fursa sawa kwa vijana, wanawake, watu wenye mahitaji maalum na makundi mengine yenye uhitaji wa fursa za kiuchumi.
Ameongeza kuwa jukumu hilo linaendana na Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, inayosisitiza kuwa mfumo wa elimu na mafunzo uzalishe watu wenye maarifa, ujuzi na umahiri unaokidhi mahitaji ya maendeleo ya Taifa na soko la ajira.
Prof. Mkenda amewataka wajumbe wa TACs kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi, ubunifu, uwajibikaji na uzalendo, akisisitiza kuwa Serikali inawategemea katika kuleta mabadiliko kwenye mfumo wa mafunzo ya ufundi stadi.
“Kwa pamoja, tuhakikishe kwamba TACs zinakuwa chachu ya mabadiliko, daraja kati ya elimu na ajira, na injini ya ubora, ubunifu na ushindani wa Taifa,” na natamka kuwa nimezindua rasmi Kamati za Ushauri wa Stadi za VETA. Amesema



Comments
Post a Comment