WANANCHI wametakiwa kujenga utamaduni wa kupima afya mara kwa mara na kutafuta huduma za kitabibu mapema, kwa kuwa saratani inaweza kutibiwa kwa ufanisi zaidi inapogundulika katika hatua za awali.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Dkt. Diwani Msemo, wakati akizungumza na waandishi wa habari leo, Agosti 19, 2026, jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa wananchi kuondokana na dhana potofu kuhusu saratani na kuchukua hatua za mapema katika afya zao.
Dkt. Msemo amesema wananchi wanapaswa kufahamu kuwa saratani si ugonjwa usiotibika, hasa pale inapogundulika mapema, huku akiviomba vyombo vya habari kuendelea kushirikiana na ORCI kutoa elimu sahihi kwa umma kuhusu kinga, uchunguzi na matibabu ya saratani.
Katika hatua nyingine, Serikali imeongeza uwekezaji mkubwa katika huduma za saratani kupitia ORCI, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuongeza uwezo wa uchunguzi na matibabu, kupunguza muda wa wagonjwa kusubiri huduma na kuimarisha nafasi ya Tanzania kuwa kituo muhimu cha huduma za saratani katika Afrika Mashariki na Kati.
Dkt. Msemo amesema uwekezaji huo unaenda sambamba na ujenzi wa vituo vipya, ununuzi na ufungaji wa vifaa vya kisasa vya uchunguzi na tiba, ukarabati wa miundombinu, pamoja na kuimarisha rasilimali watu na mifumo ya TEHAMA.
Amesema miongoni mwa miradi mikubwa ni ujenzi wa Kituo cha Saratani Mbeya, wenye thamani ya Sh bilioni 11, ambao umefikia takribani asilimia 57 na unatarajiwa kukamilika Januari 2027, huku huduma zikitarajiwa kuanza Julai mwaka huo.
Kituo hicho kinatarajiwa kuhudumia wananchi wa Mbeya na mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, pamoja na wagonjwa kutoka nchi jirani za Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Aidha, ORCI inaendelea na ujenzi wa Multipurpose Oncology Building jijini Dar es Salaam wenye thamani ya takribani Sh bilioni 5.9. Mradi huo umefikia asilimia 65 na unatarajiwa kukamilika Desemba 2026.
Kwa mujibu wa Dkt. Msemo, jengo hilo litakuwa na wodi, maeneo ya tiba ya kemikali, kliniki za saratani, maabara, famasia na ofisi za wataalamu, hatua inayolenga kupunguza msongamano na kuboresha mazingira ya wagonjwa.
Katika tiba ya mionzi, amesema ORCI imekamilisha mradi wa Linear Accelerator wenye uwekezaji wa takribani Sh bilioni 7.9, ukiwemo ujenzi na ukarabati wa chumba maalumu pamoja na ununuzi na usimikaji wa mashine hiyo.
Amesema mashine hiyo tayari imeanza kutoa huduma na inalenga kupunguza muda wa wagonjwa kusubiri kuanza matibabu hadi wastani wa takribani wiki mbili.
ORCI pia imeagiza mashine mbili za Cobalt kwa ajili ya tiba ya mionzi zenye thamani ya takribani Sh bilioni 4, huku ukarabati wa vyumba maalumu ukigharimu Sh milioni 300. Usimikaji wa mashine hizo umefikia asilimia 95 na zinatarajiwa kuanza kutumika Septemba 2026.
Kwa upande wa uchunguzi wa saratani ya matiti, Dkt. Msemo amesema ORCI imenunua mashine mbili mpya za Mammography zenye thamani ya takribani Sh bilioni 1.1. Mashine hizo zimewasili nchini na usimikaji unaendelea.
Aidha, amesema ORCI inaendelea na ufungaji wa PET Scan yenye thamani ya Sh bilioni 18.2, teknolojia inayosaidia kuonesha shughuli za viungo vya mwili, kugundua saratani na kufuatilia iwapo imeenea katika maeneo mengine ya mwili.
Amesema uwepo wa teknolojia hiyo utaongeza uwezo wa Tanzania katika uchunguzi na ufuatiliaji wa saratani na kuimarisha nafasi ya nchi katika utoaji wa huduma za kisasa za saratani barani Afrika.
Dkt. Msemo amesema taasisi hiyo pia imefunga mashine ya kisasa ya tiba ya mionzi aina ya ELEKTA Harmony, yenye thamani ya Sh bilioni 8.3, inayotumia teknolojia ya Image Guided Radiotherapy (IGRT) kusaidia kulenga eneo lenye uvimbe kwa usahihi zaidi huku ikilinda tishu na viungo vilivyo karibu.
Mashine nyingine ni SPECT, yenye thamani ya Sh bilioni 1.5, inayotumia teknolojia ya mionzi maalumu kusaidia kuonesha namna viungo vya mwili vinavyofanya kazi.
Mbali na uwekezaji katika teknolojia, amesema ORCI imeendelea kuimarisha maabara, rasilimali watu na mifumo ya TEHAMA kwa lengo la kuboresha usimamizi wa taarifa za wagonjwa na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.
Amesema taasisi hiyo pia imeimarisha huduma za uchunguzi wa mapema na kinga kupitia kampeni ya Tiba Mkoba, ambayo tayari imefika katika mikoa 15 na kuwafikia zaidi ya watu 200,000 kwa huduma za uchunguzi wa awali wa saratani.
Katika hatua nyingine, Dkt. Msemo amesema ORCI inatarajia kuanza kutoa huduma za upasuaji mkubwa wa saratani Oktoba 2026 baada ya kukamilika kwa vyumba vya upasuaji.
Amesema madaktari bingwa saba wa upasuaji tayari wamerejea nchini baada ya mafunzo, huku wataalamu wengine wanne wakiendelea na masomo.
Kwa mujibu wa Dkt. Msemo, upanuzi huo wa huduma unalenga kuifanya ORCI kuwa kituo kinachoweza kutoa huduma pana za kibingwa za saratani na kupunguza utegemezi wa wagonjwa kusafiri nje ya nchi kwa baadhi ya huduma.
Aidha, ORCI inaandaa mipango ya kuanzisha vituo vipya vya saratani katika mikoa ya Mtwara, Kigoma na Arusha, huku ikiendelea na maandalizi ya kuanzisha ORCI Consultancy Bureau, itakayotoa utaalamu katika ununuzi, usimikaji, matengenezo na matumizi ya vifaa tiba.
Dkt. Msemo amesema ORCI pia imeweka mpango wa kuwezesha uzalishaji wa dawa na bidhaa zinazotumika katika matibabu ya saratani nchini, hatua inayolenga kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje.
Amesisitiza kuwa uwekezaji huo unalenga kuimarisha huduma za kinga, uchunguzi, tiba, utafiti na mafunzo ya saratani, huku ukifungua fursa ya Tanzania kuwa kituo cha rufaa kwa wagonjwa kutoka ndani na nje ya nchi.
Hata hivyo, Dkt. Msemo amesisitiza kuwa pamoja na uwekezaji huo, hatua muhimu zaidi inaanzia kwa wananchi wenyewe—kupima afya mara kwa mara, kutambua dalili mapema na kufika hospitalini kwa wakati.
Amesema ushirikiano kati ya wananchi, wataalamu wa afya na vyombo vya habari ni muhimu katika kuongeza uelewa wa jamii na kupunguza hofu pamoja na dhana potofu kuhusu saratani.

Comments
Post a Comment