Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa nchi za Afrika kuongeza uwekezaji wa ndani katika sekta ya afya ili kujenga mifumo imara, endelevu na inayojitegemea katika usimamizi wa sekta hiyo.
Rais Dkt. Samia ametoa wito huo leo, tarehe 22 Julai, 2026 alipohutubia Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika kuhusu Afya, uliofanyika jijini Accra, nchini Ghana.
Mkutano huo umejadili namna ya kuharakisha utekelezaji wa Ajenda ya Afya ya Afrika kupitia usawa katika upatikanaji wa huduma, afya kwa wote, kutokomeza UKIMWI, kuboresha afya ya mama na mtoto, pamoja na kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza na yasiyopewa kipaumbele.
Amesema Tanzania tayari imeanza kutekeleza Ramani ya Afya ya Umoja wa Afrika 2030 kwa kuiingiza katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa 2026/2027-2030/2031, huku ikijielekeza kwenye uwekezaji katika uzalishaji wa dawa, kuimarisha mifumo ya afya na kuongeza uwezo wa nchi kujitegemea katika huduma za afya.
"Afrika ina maarifa, rasilimali watu na uwezo wa kubadili mifumo yake ya afya. Tunachohitaji sasa ni utashi mkubwa wa kisiasa, uwekezaji wa ndani na mshikamano wa bara," amesema Rais Dkt. Samia.
Aidha, amesema Serikali imefanya mageuzi ya sera na sheria ili kuvutia uwekezaji na kurahisisha biashara, hatua zilizowezesha kuanzishwa kwa viwanda 13 vya uzalishaji dawa huku wawekezaji 149 wakionesha nia ya kuwekeza nchini.
Rais Dkt. Samia pia amesema Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA) imekuwa ya kwanza barani Afrika kufikia kiwango cha tatu cha ukomavu wa mifumo ya udhibiti wa dawa wa Shirika la Afya Duniani (WHO Maturity Level 3), hatua inayotarajiwa kuharakisha uzalishaji wa dawa bora nchini na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje.
Katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya, Rais Dkt. Samia amesema Serikali imeongeza bajeti ya sekta hiyo kutoka shilingi trilioni 1.8 mwaka 2024/25 hadi shilingi trilioni 3.1 mwaka 2026/27, sambamba na kuanzisha Bima ya Afya kwa wote ili kuwawezesha wananchi, wakiwemo wenye kipato cha chini, kupata huduma muhimu za afya kwa gharama nafuu.
Amesema uwekezaji huo umewezesha kujengwa kwa hospitali za wilaya 119, vituo vya afya 649 na zahanati zaidi ya 2,700, na kuongeza idadi ya vituo vya kutolea huduma za afya kutoka takribani 10,000 hadi 13,700 kufikia mwezi Machi, 2026.
Maboresho hayo, amesema Rais Dkt. Samia, yamechangia ongezeko la uzazi unaofanyika katika vituo vya afya kutoka asilimia 65 hadi 86, na uzazi unaohudumiwa na wataalamu kutoka asilimia 66 hadi 85, huku vifo vya watoto chini ya miaka mitano vikipungua kutoka 147 hadi 43 kwa kila vizazi hai 1,000; na vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi vikipungua kutoka 556 hadi 104 kwa kila vizazi hai 100,000.
Akifungua mkutano huo, Rais wa Ghana, Mheshimiwa John Dramani Mahama, amesema kupungua kwa ufadhili wa afya duniani kunapaswa kuwa fursa kwa Afrika kuongeza uwekezaji wa ndani na kujenga mifumo ya afya inayojitegemea.
Aidha, Rais Mahama ameahidi kumuunga mkono Rais Dkt. Samia katika utekelezaji wa jukumu lake la Kinara wa Umoja wa Afrika wa Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto, akisema uongozi wa Rais Dkt. Samia utasaidia kuharakisha maendeleo katika eneo hilo.
Kadhalika, Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika na Rais wa Jamhuri ya Burundi, Mheshimiwa Évariste Ndayishimiye, amezitaka nchi wanachama kuongeza uwekezaji katika huduma za afya za msingi na kuimarisha uwezo wa bara la Afrika wa kuzuia, kugundua na kukabiliana na milipuko ya magonjwa.
Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus, alisema maazimio ya mkutano huo yatakuwa na maana ikiwa yatafuatiwa na utekelezaji madhubuti, akisisitiza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa zitakuwa msingi wa mustakabali wa afya barani Afrika.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Mheshimiwa Mahmoud Ali Youssouf, ametoa wito kwa nchi wanachama kuharakisha ujenzi wa mnyororo wa uzalishaji wa bidhaa za afya barani Afrika ili kuongeza upatikanaji wa dawa, chanjo na vifaa tiba na kuimarisha usalama wa afya wa bara.




Comments
Post a Comment