MWENGE wa Uhuru Kitaifa 2026 umezindua rasmi Mradi wa Ujenzi wa Mtambo wa Kuchuja Maji Igombe–Kabangaja mkoani Mwanza, wenye thamani ya Sh585 milioni, unaolenga kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa maeneo manne.
Mradi huo umetekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA), kwa kushirikiana na Shirika la Maji la Uholanzi, Vitens Evides International (VEI), na umekamilika kwa asilimia 100.
Uzinduzi huo umefanyika Agosti 11, 2026, wakati wa ziara ya Mwenge wa Uhuru katika Mkoa wa Mwanza, ambapo Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Mwango’nda, alisema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali na wadau wa maendeleo katika kuboresha huduma muhimu za kijamii.
Mradi huo unatarajiwa kunufaisha wananchi wa Kata za Bugogwa, Sangabuye, Kahama na Shibula, kwa kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama, hatua inayolenga kuboresha afya, usafi na ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mwango’nda alisema maji ni huduma muhimu inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, hivyo uwekezaji katika miundombinu ya maji ni hatua muhimu katika kuboresha maisha ya wananchi.
“Mradi huu ni muhimu kwa sababu unagusa maisha ya wananchi moja kwa moja. Utaongeza upatikanaji wa maji safi na salama na hivyo kuchangia kuboresha afya na ustawi wa jamii,” alisema.
Kwa mujibu wa taarifa ya MWAUWASA, utekelezaji wa mradi huo ulianza Oktoba 1, 2024 na kukamilika Juni 30, 2026.
Fedha hizo zimetumika katika ujenzi wa nyumba ya mtambo wa kuchuja maji, ununuzi na usimikaji wa tanki lenye uwezo wa kuhifadhi lita 100,000 za maji pamoja na pampu mbili zenye uwezo wa kusukuma maji lita 50,000 kwa saa.
Kazi nyingine zilizotekelezwa ni ulazaji wa bomba lenye kipenyo cha milimita 200 na urefu wa mita 12, pamoja na bomba lenye kipenyo cha milimita 100 kwa ajili ya kusafirisha maji kwenda kwenye tanki.
Mradi pia umehusisha ujenzi wa choo na uzio katika eneo la mtambo huo.
Mbali na kuboresha huduma ya maji, mradi huo umechangia shughuli za kiuchumi katika eneo hilo kwa kutoa ajira za muda kwa vijana 25 wakati wa utekelezaji wake.
Msimamizi wa Miradi wa MWAUWASA, Mhandisi Nuhu Said, alisema kukamilika kwa mradi huo kumeongeza miundombinu ya maji na kuweka msingi wa kupanua huduma kwa wananchi zaidi.
Kwa upande wake, Mratibu wa mradi kutoka VEI, Mhandisi Rukia Yunge, alisema mradi huo umeweka mazingira mazuri ya kuandaa na kutekeleza miradi mingine ya kupanua mtandao wa maji na kuongeza idadi ya wananchi watakaounganishwa na huduma hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa MWAUWASA, Mhandisi Mashaka Sitta, alisema mamlaka hiyo itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuimarisha uwekezaji kwenye miundombinu ya maji ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu.
Baada ya kuridhishwa na utekelezaji wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, pamoja na wadau wa maendeleo kwa kuwezesha utekelezaji wa miradi inayolenga kuboresha maisha ya wananchi.
Aidha, aliwataka wananchi kutunza miundombinu ya mradi huo na kuitumia kwa uangalifu ili iweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa kizazi cha sasa na kijacho.






Comments
Post a Comment