Dar es Salaam, Agosti 7, 2026
Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekutana na ujumbe kutoka African Leadership Initiative for Impact (ALI) kwa lengo la kujadili fursa za ushirikiano katika maandalizi ya Jukwaa la Amani kwa Vijana, linalotarajiwa kufanyika mwezi Septemba 2026 jijini Dar es Salaam.
Majadiliano hayo yalilenga kubaini namna pande hizo mbili zitakavyoshirikiana katika kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika kujenga amani, kukuza uongozi wenye maadili na kuimarisha mshikamano wa kijamii kupitia Elimu ya Uraia wa Dunia (Global Citizenship Education - GCED), ambayo ni moja ya maeneo ya kipaumbele ya UNESCO katika kujenga jamii zenye amani, uvumilivu na maendeleo endelevu.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Profesa Hamisi Malebo, alisema Tume imepokea kwa furaha wazo hilo na kuliona kuwa linaendana na dhamira ya UNESCO ya kujenga amani katika fikra za watu kupitia elimu, sayansi, utamaduni, mawasiliano na taarifa.
“Tume imepokea wazo hili zuri na tunaamini linaweza kuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha vijana kushiriki katika kujenga amani, kuimarisha mshikamano wa kitaifa na kuwa viongozi wa mabadiliko chanya katika jamii. Tuko tayari kuendelea na majadiliano ili kubaini maeneo ya ushirikiano yatakayowezesha kufanikisha jukwaa hili,” alisema Profesa Malebo.
Aliongeza kuwa ushirikiano huo unaendana na juhudi za UNESCO za kuhamasisha vijana kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto zinazoikabili jamii kupitia elimu, mazungumzo, uvumilivu na ushiriki wa wananchi, sambamba na kuchangia utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), hususan Lengo la 4 la Elimu Bora na Lengo la 16 la Amani, Haki na Taasisi Imara.
Kwa upande wake, ujumbe wa African Leadership Initiative for Impact ulieleza kuwa umefika Tume ya Taifa ya UNESCO ili kuwasilisha wazo la ushirikiano katika maandalizi ya Jukwaa la Amani kwa Vijana, likiwa na lengo la kuwakutanisha vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini kujadili nafasi yao katika kujenga amani, kuimarisha uongozi, kuzuia migogoro na kuchochea maendeleo endelevu.
Jukwaa hilo linatarajiwa kuwa sehemu ya kuendeleza ushirikiano kati ya taasisi mbalimbali zinazojihusisha na maendeleo ya vijana, huku likitoa fursa kwa vijana kubadilishana uzoefu, kujenga uwezo na kushiriki katika mijadala inayokuza amani na maendeleo ya Taifa.

Comments
Post a Comment