Na Mashaka Mhando, TANGA
UMOJA wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Tanga Mjini umepata ugeni mzito kutoka ngazi ya Taifa, katika ziara iliyolenga kukagua utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), hususan uwezeshaji wa wanawake kiuchumi kupitia mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Serikali.
Ziara hiyo iliyofanyika jana, Agosti 5, 2026, iliongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la UWT Taifa ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Tanga, Mhe. Husna Sekiboko.
Lengo kuu la ufuatiliaji huo ilikuwa ni kujionea kwa vitendo namna mabilioni ya fedha yanayotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yanavyoendelea kuboresha maisha ya wananchi, hasa wanawake na makundi maalum.
Ukaguzi wa Miradi ya asilimia 10
Akiwa wilayani humo, msafara wa Mhe. Sekiboko ulianza kwa kutembelea eneo la mradi wa ujenzi wa Nyumba ya Mtumishi wa UWT lililopo Mtaa wa Amboni Kihongwe, katika Kata ya Mzizima.
Baada ya hapo, viongozi hao walifanya ziara ya kukagua na kuzungumza na vikundi vya wanawake na watu wenye ulemavu vilivyonufaika na mikopo ya asilimia 10 katika kata za Chumbageni, Duga na Mabawa.
Maagizo Mazito Kikao Kikuu
Kufuatia ukaguzi huo wa miradi, kilele cha ziara kilikuwa ni kikao kikuu cha majumuisho kilichofanyika ndani ya Ukumbi wa CCM Wilaya ya Tanga Mjini.
Katika kikao hicho, Mhe. Sekiboko aliwasilisha salamu na maelekezo mahususi kutoka UWT Taifa. Aliwashukuru wanachama wa Mkoa na Wilaya ya Tanga kwa ushindi mkubwa waliokipa Chama katika Uchaguzi Mkuu, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kudumisha amani, mshikamano, na uzalendo ili kuendeleza kasi ya maendeleo.
Shukrani na Maazimio ya UWT Wilaya
Kufuatia mafanikio ya ziara hiyo, UWT Tanga Mjini imetoa shukrani za dhati kwa viongozi na wadau wote waliofanikisha mapokezi hayo.
Shukrani hizo zimeelekezwa kwa Uongozi wa UWT Mkoa wa Tanga, CCM Wilaya ya Tanga Mjini, Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi wa Jiji la Tanga kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii, pamoja na Madiwani wa Viti Maalum. Wengine ni Wajumbe wa Baraza la UWT Mkoa na Wilaya, viongozi wa Kata, Matawi, Serikali za Mitaa na wageni waalikwa wote.
Akihitimisha taarifa hiyo, Uongozi wa UWT Tanga Mjini umeahidi kutekeleza kwa vitendo maelekezo yote yaliyotolewa na viongozi wa Taifa, na kusisitiza dhamira yao ya kuendelea kuwatumikia wananchi kwa uadilifu huku wakishiriki kikamilifu kuijenga Tanga yenye maendeleo na ustawi chini ya CCM.











Comments
Post a Comment