Maendeleo ya Taifa hayaishii kwenye kuwa na sera nzuri, mipango mikubwa au dira yenye malengo makubwa lakini nyuma ya kila hatua ya maendeleo inayokusudiwa kutekelezwa, kuna msingi mmoja muhimu unaowezesha Serikali kuchukua hatua kwa uhalali, utaratibu na uwajibikaji.
Dira inaweza kuonyesha Tanzania inayotakiwa kujengwa, sera inaweza kuelekeza namna ya kufikia malengo hayo na mipango ikaainisha hatua zinazopaswa kuchukuliwa. Hata hivyo, bila mfumo madhubuti wa sheria unaoenda na wakati malengo hayo yanaweza kubaki kwenye nyaraka badala ya kugeuka kuwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.
Hapa ndipo nafasi ya Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria (OCPD) inapofanya kazi kubwa katika kufikia lengo hilo la serikali na jamii kwa ujumla. Kupitia maandalizi na uboreshaji wa sheria Ofisi hii inashiriki katika kuweka msingi wa kisheria unaosaidia Serikali kutekeleza sera, mipango na mikakati yake katika mazingira yanayobadilika kiuchumi, kijamii na kiteknolojia.
Wajibu wa OCPD katika mchakato huu ni kutafsiri na kuandika katika lugha ya kisheria maono na matakwa ya kisera ili yaweze kutekelezeka.
Akizungumzia sheria na mabadiliko hayo Mwandishi Mkuu wa Sheria Bw. Onorius Njole amesema kama sehemu ya kuendelea kuimarisha mfumo wa sheria ili kuendana na mweleke wa kisera wan chi, katika kipindi cha Januari hadi Julai 2026, OCPD kwa kushirikiana na Wizara na taasisi mbalimbali za Serikali, iliandaa miswada ya sheria saba (7) iliyolenga kutunga sheria mpya pamoja na kufanya maboresho katika sheria zilizopo.
Miswada hiyo iligusa maeneo mbalimbali yenye umuhimu katika ustawi wa Taifa ikiwemo kupanua wigo wa upatikanaji wa mikopo, biashara na uwekezaji, kilimo, kodi, ardhi, maliasili, usafiri wa anga, haki jinai, Serikali za Mitaa na matumizi ya fedha za umma. Miswada yote ilipitishwa katika Mkutano wa Nne wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliomalizika tarehe 4 Septemba 2026.
Amesema miongoni mwa Sheria hizo ni Sheria ya Mikopo kwa Dhamana za Mali Zinazohamishika ya mwaka 2026 ambayo inaweka mfumo wa kisheria unaoruhusu mali zinazohamishika kutumika kama dhamana ya mikopo na kuanzisha Masijala ya kusajili maslahi katika mali hizo.
“Hatua hii ni muhimu katika kupanua fursa za kifedha kwa watu na biashara ambazo huenda hazina mali zisizohamishika zinazokubalika kwa urahisi kama dhamana, kwahiyo kutambua mali zinazohamishika kunaweza kupanua wigo wa mali zinazoweza kutumika kupata mitaji, na hivyo kuwezesha biashara kuongeza wigo wa shughuli, uzalishaji, uwekezaji na fursa za ajira” alieleza Bw. Njole.
Aliongeza “Katika mazingira ambayo biashara na uchumi vinaendelea kubadilika, sheria nazo haziwezi kubaki palepale, hivyo kupitia Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali ya Mwaka 2026, Bunge ilimefanya maboresho katika sheria 18, huku baadhi yakilenga kuongeza uwazi katika shughuli za biashara na kuimarisha mapambano dhidi ya uhalifu wa kifedha”.
Aidha Mwandishi Mkuuu wa Sheria amesema marekebisho mengine yaliyofanyika ni katika Sheria ya Majina ya Biashara na Sheria ya Kampuni Sura ya 212.
Mabadilikoa katika sheria hii yanahusu upatikanaji na utoaji wa taarifa kuhusu umiliki manufaa. Kwa mujibu wa marekebisho haya,sasa kampuni za kigeni zinatakiwa kuwasilisha taarifa za wanahisa na umiliki manufaa kama ilivyo kwa kampuni za ndani.
Bwana Njole amesema hatua hizo zinalenga kuongeza uwazi wa umiliki wa biashara na kuimarisha mapambano dhidi ya utakatishaji fedha, ufadhili wa ugaidi na shughuli nyingine haramu.
“Maboresho hayo yamegusa pia sekta ya usafiri wa anga ambako mfumo wa uchunguzi wa ajali na matukio hatarishi ya ndege umeboreshwa ili kutambua kisheria Kitengo cha Uchunguzi wa Ajali za Ndege, masharti kuhusu uhuru wa uchunguzi, ulinzi wa taarifa nyeti na mgongano wa maslahi yanalenga kuimarisha usalama wa usafiri wa anga na kuoanisha mfumo wa Tanzania na viwango vya kimataifa” alifafanua Njole.
Katika mfumo wa haki jinai, Mwandishi Mkuu wa Sheria amesema Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya JinaiSura ya 20 imefanyiwa marekebisho ili kuondoa vikwazo vinavyoweza kuchelewesha kuanzishwa kwa taratibu za jinai pale ambapo jambo lina sura ya madai au kiutawala katika masuala ya ajira. Lengo ni kuhakikisha makosa ya jinai yanashughulikiwa kwa wakati na kwamba haki haicheleweshwi.
Bwana Njole alieleza zaidi, katika kuimarisha urekebishaji na urejeshwaji wa wafungwa katika jamii, Sheria ya Jeshi la Magereza ili kutambua elimu, mafunzo ya ufundi, huduma za kiroho na msaada mwingine kama sehemu ya kuwasaidia wafungwa wanaomaliza vifungo kurejea katika jamii.
Nae Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uandishi wa Sheria kutoka OCPD Bi. Chresencia Mathayo amesema kwa upande wa sekta ya kilimo ambayo ina nafasi muhimu katika maendeleo ya Tanzania, sheria zimepewa mwelekeo wa kusaidia kuongeza tija, ufanisi wa taasisi na ushindani wa mazao.
Amesema Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Kilimo ya Mwaka 2026 imefanya marekebisho katika sheria zinazohusu usalama wa chakula, mkonge, sukari na chai.
“Mabadiliko hayo yanalenga kuimarisha mamlaka za udhibiti, kuboresha utatuzi wa migogoro baina ya wakulima na wafanyabiashara na kupunguza muingiliano wa majukumu ya taasisi, na katika mwelekeo huo, Wakala wa Maendeleo ya Chai umefutwa na majukumu yake sasa yanatekelezwa na Bodi ya Chai hatua inayolenga kupunguza gharama za uendeshaji wa Serikali na kuongeza ufanisi” Alieleza Bi. Mathayo.
Aidha ameongeza kuwa hatua nyingine imechukuliwa ni kufuta Sheria ya Kufuta Sheria ya Tasnia ya Pareto Sura ya 376 na majukumu ya Bodi ya Pareto yaliyokuwa yameanzishwa chini ya Sheria hiyo na kuhamishiwa Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) sambamba na mali, madeni na watumishi wa Bodi huyo.
Lengo ni kupunguza uwepo wa taasisi zinazotekeleza shughuli zinazofanana, kuimarisha uratibu na kuongeza tija katika matumizi ya rasilimali za umma.
Ameongeza kuwa mabadiliko katika mfumo wa sheria yamegusa pia ardhi, maliasili na mazingira ya uwekezaji ambapo Sheria ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi imefanyiwa marekebisho ili kuimarisha ushirikiano kati ya Tume na mamlaka nyingine za upangaji wa matumizi ya ardhi na kupunguza mwingiliano wa majukumu. Adhabu nazo zimeboreshwa ili kuendana na mazingira ya sasa na kuongeza uzingatiaji wa sheria.
Mkurugenzi huyo ameeleza katika eneo la rasilimali asilia, marekebisho yamekusudia kuweka mazingira bora ya uwekezaji kwa kupanua wigo wa maeneo ambako mashauri yanayohusu migogoro ya uziduaji, uvunaji, upatikanaji au matumizi ya mali na rasilimali asilia yanaweza kusikilizwa kwa kuzingatia makubaliano ya wahusika.
Akizungumzia mabadiliko katika utawala wa Serikali za Mitaa Bi. Mathayo amesema marekebisho yameelekezwa katika kuoanisha muda wa madaraka ya viongozi wasaidizi, wakiwemo Makamu Wenyeviti na Naibu Meya, na muda wa viongozi wakuu husika, hatua inayolenga kuimarisha uwajibikaji na mwendelezo wa uongozi.
Kwa upande wa uhifadhi Wanyamapori, Bi. Mathayo amefafanua kuwa marekebisho yanapendekeza kuondoa mifugo miongoni mwa mali zinazoweza kutaifishwa baada ya mtu kutiwa hatiani kwa kosa chini ya sheria hiyo.
“Sheria ya Uthamini nayo imefanyiwa marekebisho ili kuongeza uwazi, kuweka matumizi sahihi ya misingi ya uthamini na kuhakikisha shughuli za kitaalamu zinafanywa na watu waliosajiliwa au kutambuliwa kwa mujibu wa sheria” Alieleza Bi. Mathayo.
Aliongeza “Katika upande wa uchumi na utekelezaji wa bajeti, Sheria ya Fedha ya mwaka 2026 imefanya marekebisho katika sheria 26 za kodi na zisizo za kodi, mabadiliko hayo yanahusu baadhi ya kodi, tozo na ada, pamoja na hatua za kuimarisha ukusanyaji na usimamizi wa mapato na kuboresha mazingira ya biashara”.
Mkurugenzi huyo wa Uandishi wa Sheria amesema marekebisho hayo yanalenga pia kuchochea ukuaji wa uchumi katika sekta za kimkakati zikiwemo viwanda, kilimo, nishati na afya.
“Maboresho haya yanatoa ujumbe mpana zaidi kuhusu nafasi ya sheria katika maendeleo ya Taifa. Sheria bora inapaswa kutoa uhakika, kulinda haki, kuweka uwajibikaji, kuondoa vikwazo visivyo vya lazima na kufungua fursa za maendeleo. Hivyo basi, miswada iliyoshughulikiwa katika kipindi cha Januari hadi Julai 2026 ni zaidi ya marekebisho ya vifungu vya sheria.
Ni sehemu ya safari ya kujenga mfumo wa sheria unaoendana na mahitaji ya Tanzania ya sasa na unaoweka msingi wa Tanzania inayokusudiwa kujengwa katika miongo ijayo”. alibainisha Bi. Chresencia.



Comments
Post a Comment