Na Ghati Msamba, Musoma.
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mara, Agnes, ametoa elimu kwa wasafirishaji wa bodaboda na bajaji kuhusu fursa za mikopo inayolenga kuwawezesha kupata vitendea kazi na kujikwamua kiuchumi, huku akiwataka kutumia fursa hizo kwa uaminifu na kurejesha mikopo kwa wakati.
Akizungumza katika mkutano na wasafirishaji hao, Mbunge Agnes alisema mikopo hiyo ni miongoni mwa fursa zinazolenga kuwawezesha vijana kuongeza kipato, kuboresha maisha yao na kutoka katika kiwango cha chini cha kiuchumi kwenda kwenye kiwango cha kati.
Alisema vijana hao wana nafasi ya kunufaika na mabilioni ya fedha yanayotolewa kupitia programu mbalimbali za kuwawezesha kiuchumi, ikiwemo kupata bodaboda na bajaji zitakazowawezesha kujiajiri na kuongeza kipato.
Mbunge huyo alisema anajivunia kuwa sehemu ya jitihada za kuwawezesha vijana, akieleza kuwa ana faraja kubwa kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan katika juhudi za kuinua wananchi kiuchumi.
“Rais Samia amefanya mambo mengi katika kuwawezesha wananchi. Mimi mwenyewe ni mmoja wa watu ambao nimepata faraja kutokana na fursa zilizopo, kwani zamani nilikuwa muuza dagaa. Leo nimepata nafasi ya kuwa mbunge na ninapaswa kutumia nafasi hii kuwahudumia wananchi,” alisema.
Aidha, aliwataka wanufaika wa mikopo hiyo kuwa waaminifu kwa kuhakikisha wanarejesha fedha walizokopa kwa wakati, ili kuwapa nafasi wananchi wengine kupata mikopo hiyo na wao wenyewe kuweza kukopa tena pale wanapohitaji.
Alisema urejeshaji wa mikopo ni muhimu kwa sababu fedha hizo zinapozunguka huwezesha watu wengi zaidi kunufaika na programu hizo.
Mbunge Agnes pia aliwataka wasafirishaji hao kutosikiliza taarifa za upotoshaji kutoka kwa baadhi ya watu wanaowashauri kutorejesha mikopo kwa madai kwamba mikopo hiyo ni sehemu ya siasa.
“Msidanganywe na watu wanaowaambia msirejeshe mikopo kwa sababu eti ni siasa. Mkopo ni wajibu na unapaswa kurejeshwa ili wengine nao wapate fursa. Tukitumia vizuri fursa hizi, tunaweza kubadilisha maisha yetu,” alisema.
Kwa upande mwingine, Mbunge Agnes alisema amebaini kuwa baadhi ya wasafirishaji katika eneo hilo wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya ukosefu wa vitendea kazi, hali inayowafanya washindwe kuongeza kipato na kuboresha maisha yao.
Alisema lengo la kuwafikishia elimu kuhusu mikopo hiyo ni kuhakikisha wanapata uelewa sahihi wa taratibu, masharti na namna bora ya kutumia mikopo hiyo katika shughuli za uzalishaji.
Akizungumzia kauli za baadhi ya watu wanaodai kuwa anatumia shughuli hizo kufanya kampeni, Mbunge Agnes alisema yeye ni mwakilishi wa wananchi aliyechaguliwa na ana wajibu wa kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Ilani ya Chama chake.
“Tuache propaganda za watu wanaosema Agnes anafanya kampeni. Mimi ni mbunge niliyechaguliwa na wananchi, hasa akina mama, na ninafanya kazi niliyotumwa. Nataka niache alama katika kuwahudumia wananchi,” alisema.
Aliongeza kuwa viongozi wanapaswa kuwatumikia wananchi kwa vitendo kwa kuwa wananchi ndio waliowapa dhamana ya kuwaongoza.
“Tunapaswa tuwahudumie wananchi kwa sababu mlituchagua ili tuwahudumie. Mimi sihitaji maneno mengi, ninachotaka ni kuona wananchi wanapata huduma na fursa zinazoweza kubadilisha maisha yao,” alisema.
Kwa upande wake, Afisa Mikopo kutoka Benki ya CRDB, Samwel, aliwataka wasafirishaji hao kutumia vizuri fursa hiyo ya mikopo na kuhakikisha wanatimiza masharti yaliyowekwa, ikiwemo kurejesha mikopo kwa wakati.
Samwel pia alimpongeza Mbunge Agnes kwa kuwashirikisha wananchi katika fursa hizo, akisema wapo baadhi ya watu wanaopata fursa za kiuchumi lakini hawako tayari kuwashirikisha wengine.
“Tunapaswa kumshukuru Mbunge Agnes kwa sababu kuna watu wengine wanapata fursa kama hizi lakini wanakuwa wagumu kuwashirikisha wananchi. Anapopatikana mtu anayewafikishia wananchi fursa na elimu kama hii, anapaswa kupewa pongezi,” alisema.
Aliwataka wasafirishaji hao kuchangamkia fursa hiyo kwa kuzingatia masharti ya mikopo na kutumia fedha kwa malengo yaliyokusudiwa, ili waweze kukuza shughuli zao za usafirishaji na kuongeza kipato.
Mkutano huo umeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kuwafikishia vijana taarifa kuhusu fursa za uwezeshaji kiuchumi, hususan mikopo inayoweza kuwasaidia kupata vitendea kazi na kujenga uwezo wa kujitegemea kupitia shughuli za usafirishaji.









Comments
Post a Comment