Na Dawati la Habari Polisi Mwanza
Jeshi la Polisi Wilaya ya Nyamagana limewataka vijana kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani na usalama wa jamii kwa kushirikiana kwa karibu na vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na serikali za mitaa katika kuwabaini na kuwafichua wahalifu wanaojificha kwenye maeneo yao.
Wito huo umetolewa Julai 26, 2026 na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Nyamagana, SSP Virginia Sodoka, wakati wa fainali za mashindano ya Polisi Jamii Cup zilizofanyika katika Kata ya Mirongo, ambapo Mashi FC ilitwaa ubingwa baada ya kuifunga Mirongo FC mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Mirongo.
Akizungumza mbele ya mamia ya wananchi na mashabiki wa soka waliojitokeza kushuhudia fainali hizo, SSP Sodoka alisema vijana ni nguvu kazi ya taifa na nguzo muhimu katika kuhakikisha mfumo wa Polisi Jamii unafanikiwa.
"Vijana wana nafasi kubwa ya kuwa walinzi wa amani katika jamii. Mkiamua kushirikiana na Jeshi la Polisi mtasaidia kuzuia uhalifu kabla haujatokea. Lakini pia msipokuwa makini, mnaweza kutumiwa na watu wenye nia ovu kuvuruga usalama. Tunawahimiza mchague kuwa sehemu ya suluhisho, si sehemu ya tatizo," alisema SSP Sodoka.
Alisema usalama wa nchi huanzia katika ngazi ya familia, mtaa na kijiji, hivyo ushiriki wa wananchi, hususan vijana, ni msingi wa mafanikio ya juhudi za kupambana na uhalifu.
Mbali na kuhamasisha usalama, SSP Sodoka alisema mashindano ya Polisi Jamii Cup yameendelea kuwa daraja muhimu la kuimarisha uhusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi, huku yakitoa fursa kwa vijana kuonyesha vipaji vyao, kujenga nidhamu, kukuza mshikamano na kujifunza kuhusu fursa za maendeleo na ujasiriamali.
Kwa upande wake, Polisi Kata wa Mirongo, Mkaguzi wa Polisi Fatuma Mpinga, alisema michezo imeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuwaunganisha vijana na kuwajengea utamaduni wa ushirikiano na kuheshimu sheria.
"Kupitia mashindano haya tunawafikia vijana kwa urahisi, tunawapa elimu ya usalama na kuwajengea moyo wa kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia vitendo vya uhalifu," alisema Mkaguzi Mpinga.
Naye Diwani wa Kata ya Mirongo, Nurdin Anas Baji, aliipongeza Kamandi ya Polisi Mkoa wa Mwanza kwa kuanzisha mashindano hayo, akisema yamekuwa chachu ya kuimarisha mshikamano na amani katika jamii.
Aliwataka vijana kuendelea kutumia michezo kama nyenzo ya kujenga umoja, kuibua vipaji na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha mustakabali wao.
Baadhi ya wachezaji walioshiriki mashindano hayo, akiwemo Anod Petar na Muzaifa Mudabiru, walilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuandaa mashindano hayo na kuomba yawe endelevu ili vijana wengi zaidi wanufaike na fursa za michezo pamoja na elimu ya usalama.
Mashindano ya Polisi Jamii Cup ni sehemu ya mkakati wa Jeshi la Polisi wa kuimarisha ushirikiano na wananchi kupitia michezo, kwa lengo la kuendelea kudumisha amani, usalama na mshikamano katika jamii.













Comments
Post a Comment