Na Prosper Makene
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeiomba jamii ya kimataifa kuipa lugha ya Kiswahili heshima yake kama lugha ya umoja, ujumuishaji na utambulisho wa Kiafrika.
Hayo yamesemwa na Mhe. Balozi Dkt. Hoyce Temu, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa na Mashirika mengine ya Kimataifa nchini Uswis, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Watu Wenye Asili ya Afrika yaliyofanyika Geneva hivi karibuni.
Balozi Dkt. Temu amesema lugha ina mchango mkubwa katika kulinda urithi, utu na haki za watu.
Mkutano huo uliandaliwa na Chuo cha Uma cha Kiafrika Uswisi, UPAF, pamoja na washirika wengine.
Balozi Dkt. Temu amewashukuru UPAF kwa kazi nzuri wanayofanya ya kukuza utamaduni wa Kiafrika kupitia Mradi wa Kiswahili.
Amesema kwa Tanzania, Kiswahili ni zaidi ya lugha ya mawasiliano. “Ni lugha ya umoja wa Kiafrika, utambulisho, amani na ushirikiano kati ya nchi. Inaunganisha watu wengi kuvuka mipaka. Leo hii inatumika pia katika diplomasia, elimu, utamaduni na ushirikiano wa kimataifa,” amesema.
Balozi Dkt. Temu ameongeza kuwa Tanzania inajivunia Kiswahili lakini pia inatambua na kuheshimu lugha nyingine za Afrika kama Kihausa, Kiyoruba, Kioromo na nyingine nyingi. Amesema kusukuma Kiswahili mbele sio kupuuza lugha nyingine, bali ni sehemu ya kuhakikisha lugha zote za Afrika zinapata heshima duniani.
Akizungumzia mafanikio yaliyopatikana chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Balozi Dkt. Temu amebainisha kuwa kumekuwa na hatua kubwa katika kueneza Kiswahili kimataifa.
Mwaka 2021, UNESCO ilitangaza tarehe 7 Julai kuwa Siku ya Lugha ya Kiswahili Duniani. Mwaka 2022, Kiswahili kilipata kutambuliwa zaidi na Umoja wa Afrika. Mwaka 2024, Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulipitisha Azimio Namba A/RES/78/312 la kutangaza tarehe 7 Julai kuwa Siku ya Lugha ya Kiswahili Duniani. Na mwaka 2025, Mkutano Mkuu wa UNESCO ulikubali Kiswahili kuwa lugha rasmi ya saba ya shirika hilo.
Baada ya hatua hizo, Tanzania imeomba Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa uone uwezekano wa kutambua Kiswahili kama lugha rasmi ya saba ya Umoja wa Mataifa.
Balozi Dkt. Temu amesema: “Kiswahili kinazungumzwa na watu zaidi ya milioni 200. Tayari kimetambuliwa na mashirika makubwa ya Afrika na kimataifa. Je, kinatakiwa kungojea kwa muda gani zaidi na nini kingine kinahitajika ili kiwe lugha rasmi ya Umoja wa Mataifa?”
Amesema suala hili halihusu lugha peke yake. “Ni suala la kujumuisha watu, la uwakilishi, la utu na heshima ya kitamaduni, na la nafasi ya Afrika katika taasisi za dunia.”
Kwa sababu hiyo, Tanzania imewaomba Umoja wa Afrika, nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, mashirika ya kiraia, vyuo vikuu na washirika wengine kuendelea kuunga mkono jitihada za kuinua Kiswahili. Lengo ni kutoka kuwa “lugha ya umoja wa Kiafrika” na kuwa “lugha ya diplomasia ya kimataifa”.
Balozi Dkt. Temu amehitimisha kwa kusema kuwa chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tanzania itaendelea kutumia Kiswahili kama sehemu ya diplomasia ya kitamaduni na kujitolea kwake kuutangaza utambulisho wa Kiafrika duniani.

Comments
Post a Comment