Na Mwanamkuu Mwandoro, Mkinga
Serikali imeendelea kuonesha dhamira yake ya kusikiliza maoni ya wananchi katika kutafuta suluhisho la kudumu la mgogoro wa Shamba la Manza-Bay, lililopo Kijiji cha Boma Kichakamiba, Kata ya Boma, Wilaya ya Mkinga, kwa kuahidi kuyafanyia kazi maoni yaliyotolewa kupitia taratibu za Serikali.
Kauli hiyo imetolewa Julai 24, 2026 na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Dkt. Balozi Batilda Burian, wakati wa kikao cha kusikiliza maoni ya wananchi kuhusu mgogoro huo. Amesema Serikali inatambua umuhimu wa kuwashirikisha wananchi katika maamuzi yanayogusa maisha yao na kwamba maoni yote yaliyotolewa yatapewa uzito unaostahili ili kufikia suluhisho la haki na la kudumu lenye kuzingatia maslahi ya wananchi pamoja na mwekezaji.
"Serikali imekuja kuwasikiliza wananchi. Maoni yenu ni sehemu muhimu ya mchakato wa kupata suluhisho la kudumu, na yatafanyiwa kazi kwa kuzingatia sheria, haki na maslahi ya pande zote," amesema Mhe. Dkt. Burian.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mkinga, Mhe. Gilbert Sylvester Kalima, amesema ujio wa Mkuu wa Mkoa ni utekelezaji wa maelekezo ya viongozi wa ngazi za juu, ikiwemo timu ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, yenye lengo la kuhakikisha mgogoro huo unatatuliwa kwa njia ya mazungumzo na ushirikishwaji wa wananchi.
Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuweka mbele maslahi ya wananchi na kuhakikisha kila upande unasikilizwa ili kufikia muafaka utakaodumu.
Katika kikao hicho, wananchi walipata fursa ya kutoa maoni yao na kueleza mapendekezo mbalimbali kuhusu namna bora ya kutatua mgogoro huo. Miongoni mwao, Bi. Yusta Kayombo aliiomba Serikali kuendelea na mazungumzo yatakayowezesha kupatikana kwa suluhisho la kudumu litakalowawezesha wananchi kuendelea na shughuli za kilimo, huku akisisitiza kuwa wanatambua umiliki halali wa shamba hilo na mwekezaji.
"Mhe. Mkuu wa Mkoa, tunatambua kuwa umiliki halali wa shamba hili ni wa mwekezaji, lakini tunaiomba Serikali iendelee na mazungumzo na kuja na suluhisho la kudumu litakalotuwezesha wananchi kuendelea na shughuli za kilimo kwa sababu ni chanzo kikuu cha maisha yetu".Amesema Bi. Kayombo
Shamba la Mkonge la Manza-Bay linaundwa na mashamba manne ambayo ni Shamba Na. 196 lenye Hatimiliki Na. 14322, Shamba Na. 272 lenye Hatimiliki Na. 3576, Shamba Na. 273 lenye Hatimiliki Na. 7047 pamoja na Shamba lenye Hatimiliki Na. 14275. Mashamba hayo yana jumla ya ukubwa wa ekari 2,217.6 na yanamilikiwa na Kampuni ya Mbegu Technologies Inc. Limited.
Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa katika kikao hicho, mashamba hayo yalinunuliwa kutoka Benki ya CRDB tarehe 14 Aprili 2004 kupitia mnada wa hadhara kwa ajili ya uwekezaji wa kilimo cha kisasa. Hata hivyo, baadaye baadhi ya wananchi kutoka vijiji vinavyozunguka eneo hilo waliingia na kuanza kufanya shughuli za kilimo, hali iliyoibua mgogoro unaoendelea kushughulikiwa na Serikali.







Comments
Post a Comment