Na. Mohammed Ulongo
Katika kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari nchini, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) pamoja na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), zimetangaza kuwa jumla ya kazi 294 zimefuzu hatua ya mwisho ya Tuzo za Uandishi wa Habari na Makala za Maendeleo za Samia Kalamu Awards 2026.
Akizungumza leo Septemba 3, 2026 jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Samia Kalamu Awards 2026, Mhandisi Peter P. Mwasalyanda, amesema mkutano huo na waandishi wa habari ulikuwa na lengo la kuwaeleza wananchi namna ya kushiriki katika zoezi la kupiga kura kwa ajili ya kuwapata washindi wa tuzo hizo.
Mhandisi Mwasalyanda amesema katika hatua za awali, waandaaji walipokea jumla ya kazi 3,003 zilizowasilishwa na waombaji 985 kutoka maeneo mbalimbali nchini, ambapo baada ya kupitia mchakato wa tathmini, majaji walifanikiwa kuteua kazi 294 ambazo sasa zimefika hatua ya kupigiwa kura na wananchi.
Amesema zoezi la upigaji kura limeanza leo Septemba 3, 2026 na linatarajiwa kuhitimishwa Septemba 30, 2026, huku wananchi wakipewa fursa ya kupiga kura kupitia tovuti ya www.samiaawards.tz au kwa kutuma ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) wenye neno “SKA” likifuatiwa na namba ya mshiriki kwenda namba 15200.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti Mwenza wa Samia Kalamu Awards 2026, Dkt. Rose Reuben, amesema wananchi wana wajibu wa kushiriki kikamilifu katika zoezi hilo kwa kuzipigia kura kazi wanazoziona zina ubora, kwa kuwa ushiriki wao ni sehemu muhimu ya kuendeleza na kukuza maudhui yanayotengenezwa na waandishi wa habari nchini.
Dkt. Reuben amesema tuzo hizo pia zina nafasi ya kuibua na kuhamasisha vipaji vya waandishi wa habari, huku zikitoa jukwaa kwa kazi zenye ubunifu, utafiti na maudhui yenye mchango katika jamii kutambulika ndani na nje ya Tanzania.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Prudence Costantine, amesema matarajio ya waandaaji wa tuzo hizo ni kuona ushindani unaojengwa kupitia tuzo hizo ukichochea kuimarika kwa maadili, weledi, ubunifu na matumizi ya utafiti katika kazi za waandishi wa habari.
Naye Beatrice Bandawe, mwakilishi wa majaji wa tuzo hizo, amesema katika tathmini iliyofanywa na jopo la majaji wamebaini kuwa waandishi wa habari nchini wana uwezo mkubwa wa kuibua na kuwasilisha masuala mbalimbali ya maendeleo, hususan katika sekta za uchumi na mazingira.
Ushiriki wa wananchi katika hatua hii unatarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kuamua kazi zitakazong’ara zaidi katika tuzo hizo, huku kila kura ikiwa na nafasi ya kumsaidia mwandishi au kazi fulani kufikia ushindi. Hivyo, wananchi wanahimizwa kutumia fursa hiyo kusoma, kusikiliza au kufuatilia kazi zilizoteuliwa na kutoa kura zao kwa kazi wanazoamini zimeleta mchango chanya kwa jamii.
Samia Kalamu Awards 2026 pia inatajwa kuwa jukwaa muhimu la kuendelea kujenga kizazi cha waandishi wanaoweza kutumia kalamu, kamera na majukwaa ya kidijitali kuibua changamoto, kutoa elimu na kusimamia masuala yenye umuhimu kwa maendeleo ya taifa.
Kwa kuzingatia idadi ya kazi 3,003 zilizowasilishwa katika hatua za awali, hatua ya mwisho ya tuzo hizo inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa, huku macho ya wadau wa habari na wananchi yakielekezwa kwenye kazi 294 zilizofuzu. Zoezi la upigaji kura litakamilika Septemba 30, 2026, ndipo mchakato utaelekea kwenye hatua za mwisho za kuwatangaza washindi.














Comments
Post a Comment