Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amekutana na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS), Mhe. Moussa Saleh Batraki, katika mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na OACPS pamoja na kuharakisha utekelezaji wa ajenda ya mageuzi ndani ya Jumuiya.
Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 20 Julai 2026, Waziri Kombo amesisitiza kuwa Tanzania itaendelea kuunga mkono mageuzi yanayolenga kuifanya OACPS kuwa taasisi yenye ufanisi, uwajibikaji na uwezo mkubwa wa kuhudumia nchi wanachama.
Aidha, Waziri Kombo ameeleza umuhimu wa OACPS kuwa daraja na kiungo muhimu cha kuimarisha ushirikiano kati ya nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki, pamoja na kuwa na usimamizi bora wa rasilimali na utekelezaji wenye matokeo wa programu za Jumuiya ili kuongeza imani ya nchi wanachama na washirika wa maendeleo.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa OACPS, Mhe.Batraki, ameishukuru Tanzania kwa uongozi wake, mchango wake katika shughuli za Jumuiya na uungwaji mkono wake kwa ajenda ya mageuzi. Amesema anaithamini nafasi ya Tanzania katika kuendeleza malengo ya OACPS na kuimarisha mshikamano wa nchi wanachama.
Vilevile, Mhe. Batraki amepongeza mchango wa Tanzania katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa, huku akieleza dhamira yake ya kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo endelevu kwa manufaa ya nchi wanachama wa OACPS.















Comments
Post a Comment