Skip to main content

@marato_tv

@marato_tv
#sauti_ya_jamii

SERIKALI YAFAFANUA SHILINGI BILIONI 730 ZA MPANGO WA KUKABILI EL-NIÑO


 SERIKALI imefafanua kuwa makadirio ya Shilingi bilioni 730 yanayotajwa katika Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El-Niño si fedha zilizotengwa na Serikali kwa matumizi ya moja kwa moja, bali ni makadirio ya rasilimali zinazohitajika kutekeleza mpango huo kwa kushirikisha Serikali, taasisi, sekta binafsi, mashirika ya kitaifa na kimataifa pamoja na wadau wengine. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi, amesema mpango huo umeandaliwa kufuatia utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) wa Agosti 18, 2026, uliotabiri uwepo wa El-Niño yenye nguvu inayoweza kusababisha mvua kubwa, mafuriko, maporomoko ya ardhi, magonjwa ya mlipuko kwa binadamu na wanyama pamoja na madhara kwa miundombinu, makazi na shughuli za kiuchumi. 

Amesema mpango huo umeandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikisha Wizara, Idara na Taasisi za Serikali, Mikoa na Halmashauri, mashirika ya kitaifa na kimataifa, Umoja wa Mataifa na Asasi zisizo za Kiserikali, kwa kuzingatia Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa.

Kwa mujibu wa Prof. Kabudi, makadirio ya Shilingi bilioni 730 yamezingatia ukubwa wa madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na El-Niño ya mwaka 2026/27, uchambuzi wa madhara kwa sekta mbalimbali pamoja na uzoefu wa madhara yaliyosababishwa na matukio ya El-Niño ya miaka ya 2023/24, 2015/16 na 1997/98.

“Fedha zilizotengwa katika bajeti ya Serikali ya mwaka 2026/27 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli hizo kwa sekta zote ni Shilingi bilioni 10,” amesema Prof. Kabudi, akisisitiza kuwa kiasi cha Shilingi bilioni 730 ni makadirio ya rasilimali zinazohitajika kutoka kwa wadau mbalimbali katika kutekeleza shughuli zilizoainishwa kwenye mpango.

Amesema baadhi ya shughuli hizo tayari zinaendelea kutekelezwa na sekta na wadau mbalimbali kupitia bajeti zao za mwaka wa fedha 2026/27, kulingana na vipaumbele vya kuzuia na kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.

Mpango huo umejikita katika ukarabati na uboreshaji wa miundombinu ikiwemo barabara, madaraja, reli, mitaro, makalvati pamoja na miundombinu ya afya, elimu, usafiri, nishati ya umeme, maji safi, maji taka na mawasiliano katika maeneo hatarishi.

Aidha, Serikali imepanga kuimarisha hifadhi ya akiba ya chakula, kuhakikisha vifaa vya uokoaji na misaada ya kibinadamu vinapatikana katika maghala ya kikanda, kuandaa maeneo salama ya makazi ya muda na kutoa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kuzuia na kupunguza madhara ya mafuriko, radi, maporomoko ya ardhi na magonjwa ya mlipuko.

Serikali pia imeagiza maeneo hatarishi yatambuliwe mapema, tathmini za vihatarishi zifanyike na wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi wahamasishwe kuhamia maeneo salama endapo kutakuwa na tishio la maafa.

Katika sekta ya afya, mifugo na kilimo, mamlaka zimeelekezwa kuandaa mipango ya kuzuia milipuko ya magonjwa kwa binadamu, wanyama na mimea.

Wizara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri zimeagizwa kufanya ukaguzi na kuimarisha miundombinu muhimu, hususan madaraja, makalvati na mitaro, huku usimamizi wa mazingira ukiimarishwa kwa kudhibiti taka ngumu, kusafisha njia za maji na kuimarisha kingo za mito na mabwawa.

Serikali pia imewataka wananchi kutumia fursa ya mvua hizo kwa shughuli za uzalishaji, ikiwemo kilimo, ufugaji, uvunaji wa maji na uvuvi, huku wakitumia mbinu bora za kilimo na kuchagua mazao pamoja na mbegu zinazofaa kwa msimu wa Vuli.

Prof. Kabudi ametoa wito kwa vyombo vya habari na wadau wote kutoa taarifa sahihi kuhusu mpango huo ili kuondoa taharuki na kusaidia jamii kuelewa hatua zinazochukuliwa kabla, wakati na baada ya kutokea kwa majanga.

Amesema Ofisi ya Waziri Mkuu, kupitia maelekezo yaliyotolewa Agosti 26, 2026, imewaelekeza Wakuu wa Mikoa yote ambayo kwa mujibu wa utabiri inaweza kuathiriwa na mvua za El-Niño kuchukua hatua za maandalizi na kukabiliana na madhara yanayoweza kujitokeza.

Aidha, wananchi wametakiwa kuendelea kufuatilia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na TMA na kutoa taarifa kwa mamlaka husika kwa wakati pindi maafa yanapotokea.

“Usimamizi wa maafa ni jukumu letu sote, shiriki sasa na chukua hatua,” amesisitiza Prof. Kabudi.





Comments

#maratotv

RAIS RUTTO AAMBATANA NA ODINGA NCHINI CHINA

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mh William Rutto na mke wake wamewasili nchini China kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi na Serikali wa Jukwaa la ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC). Katika ziara hiyo ameambatana na waziri mkuu mstaafu wa nchi hiyo Raila Odinga ambaye pia anapigiwa kampeni ili aweze kushinda nafasi ya Uenyekiti wa AU.

WIZARA YA MALI ASILI YASISITIZA MATUMIZI YA SHERIA NA KANUNI KATIKA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI ZA UHIFADHI

Na.Joyce Ndunguru, Morogoro. Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii anaeshughulikia Maliasili, Kamishna wa Polisi Benedict Wakulyamba asisitiza matumizi ya sheria na kanuni katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za uhifadhi. Kamishna Wakulyamba ameyasema hayo leo Septemba 1, 2024 wakati wa ziara ya kikazi aliyoifanya katika ofisi za Makao Makuu ya TAWA yaliyopo Mkoani Morogoro kwa lengo la kuongea na watumishi ili kuimarisha utendaji kazi pamoja na kukagua maeneo ya kazi. "Kama wahifadhi tunapaswa kufahamu sheria zote zinazosimamia masuala ya uhifadhi zilizopo katika Taasisi zetu pamoja na za Taasisi zingine za uhifadhi zilizopo ndani ya Wizara ya Maliasili na utalii" amesema Kamishna Wakulyamba. "Pamoja na kufahamu sheria na kanuni zilizopo ndani ya Wizara yetu, ni vyema kufahamu na kuzingatia sheria nyingine za Nchi ambazo zinatuzunguka ili ziweze kutusaidia katika utekelezaji wa majukumu yetu mfano sheria inayohusiana na ukusanyaji wa vielelezo kuanzia kw...

Rais Dkt. Samia Awasili China Kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano Kati ya China na Africa FOCAC

  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Beijing Capital nchini China kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) tarehe 03 Septemba, 2024.

MAKOMANDOO MIAKA 60 YA JWTZ,HAIJAWAHI KUTOKEA

Makomandoo ya jeshi la ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ)wamekuwa kivutio cha aina yake kwenye kikele cha maadhimisho ya miaka 60 ya tangu kuanzishwa kwa jeshi hilo. Katika sherehe hizo ambazo zimefanyika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshiriki kwenye kilele cha Maadhimisho ya Miaka 60 ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika uwanja huo wa Uhuru Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 1 Septemba, 2024. Rais ameonesha kujivunia na kulipongeza JWTZ kwa kufanya kazi kwa kufuata misingi ya kuanzishwa kwake huku akitumia nafasi hiyo kuwapongeza Marais waliomtangulia kwa kazi kubwa waliyofanya wakati wa uongozi wao kwa kuliongoza vema jeshi hilo.

Meli ya Mv. Serengeti yapinduka na kuzama katika Bandari ya Mwanza kusini

 Meli Mv.Serengeti imepinduka na kuzama kwenye bandari ya mwanza kusini.  Meli hiyo imepinduka na kuzama disemba 26 majira ya saa Saba za usiku.  Tukio hilo limetokea meli hiyo ikiwa imefungwa katika gati la bandari ya mwanza kusini.  Kampuni ya meli Tanzania(Tashico) imethibitisha meli ya Mv. Serengeti kupinduka na kuzama upande mmoja wa nyuma.  Kwa Mujibu wa Taarifa iliyotolewa na kitengo cha Masoko na Uhusiano kwa Umma cha Kampuni hiyo inaeleza kuwa Tashico imeshirikiana na Timu mbalimbali za Wataalam kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania(TASAC), Mamlaka ya Usimamizi wa bandari (TPA) na wadau wengine katika Juhudi za Uokoaji.  Kwa Mujibu wa Taarifa hiyo,Taarifa rasmi ya chanzo cha Tatizo itatolewa Meli hiyo itakapokuwa imeinuliwa na Uchunguzi wa kubaini Tatizo utakapokuwa umefanyika. Meli ya Mv.Serengeti inadaiwa kusitisha safari zake kwenye ziwa Victoria mwaka 2016  Meli ya Mv.Serengeti imepinduka na kuzama katika...

Jenerali Jacob Mkunda Atembelea Meli Tiba ya China Aridhishwa na Huduma

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Jacob John Mkunda ametembelea meli tiba ya Jeshi la Ukombozi la Watu wa China Peace Ark ili kuona matibabu yanavyofanyika. Jenerali Mkunda amefurahishwa na namna wataalam wa tiba wa Jeshi la China walivyotoa matibabu kwa kushirikiana na wataalam wa tiba wa JWTZ . Meli tiba ya jeshi la China imekuja hapa nchini na kutia nanga kwenye bandari ya Dar Es Salaam kutoa matibabu mbalimbali kwa wananchi ikiwa ni muendelezo wa maadhimisho ya miaka 60 tangu kuanzishwa kwa JWTZ  na ushirikiano wa miaka 60 baina ya JWTZ na Jeshi la Ukombozi la Watu wa  China. Matibabu hayo yalianza kutolewa tarehe 18 Julai 2024 hadi tarehe 22 Julai 2024. Meli tiba hiyo itaondoka hapa nchini tarehe 23 Julai mwaka huu.

AMIRI JESHI MKUU AKAGUA GWARIDE LA MIAKA 60 YA JWTZ

 Mapema leo asubuhi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Mhe.Dkt,Samia Suluhu Hassan akikagua Gwaride Maalumu la Maadhimisho ya Miaka 60 ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Uwanja wa Uhuru leo September 01,2024. Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza kuwa jeshi la ulinzi la Wananchi Tanzania si jeshi la Uvamizi bali ni jeshi la ulinzi wa Wananchi Tanzania Amewahakikishia wanajeshi kufanya kazi kifua mbele,kuwa amiri jeshi mkuu yuko pamoja nao wakati wote.

Mbunge wa Bukoba Vijijini ameaga Sifa Kedekede Kwa Rais Samia

 Na Angela Sebastian; Bukoba  MBUNGE wa jimbo la Bukoba vijijini Dk. Jasson Rweikiza amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya wananchi wa jimbo hilo, kwa kuwapatia zaidi ya shilingi bilioni 19 kwa ajili ya ujenzi wa madaraja mawili ambayo ni lango la kutoka na kuingia ndani ya mkoa wa Kagera. Ametoa shukrani hizo wakati akiongea wananchi mbalimbali waliofika katika viwanja vya Rweikiza pre and Primary school iliyoko eneo la Kyetema Bukoba vijijini, kwa kwa ajili ya kumbukizi ya miaka 100 ya kuzaliwa baba wa mbunge huyo aliyekuwa akiitwa Samsoni Rweikiza.  Rweikiza amebainisha kuwa,Dk. Samia Suluhu Hassan ni Rais mwenye upendo amekubali kutoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya Bukoba Vijijini na ndiyo maana tunasema atakuwa kiongozi wetu kwa awamu nyingine tena,tunapaswa kila mmoja kumuunga mkono. ametaja madaraja hayo kuwa ni Karebe ambalo limetengewa kiasi cha shilingi bil.9.3 kwa ajili ya ukarabati mkubwa kutokana na daraja ...

Jenerali ameacha alama ya uzalendo na kujitoa kwa ajili ya Taifa

*📌 Serikali itaenzi na kuthamini mchango wake* *📌 Asema Jenerali Musuguri alijitolea kuhakikisha Tanzania inabaki na amani na usalama* *📌 Asema alikuwa mstari wa mbele kuliokoa Taifa* *📌 Aiasa jamii kuacha alama katika maisha ya kila siku* *📌 Dkt. Biteko aongoza mamia ya watu mazishi ya Jenerali Musuguri Butiama* Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa  aliyewahi kuwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Mstaafu David Bugozi Musuguri alijitolea  kuhakikisha Tanzania inabaki kuwa na amani, usalama na mshikamano pamoja na kuifundisha jamii  moyo wa dhati wa kuilinda nchi. Dkt. Biteko amesema hayo leo Novemba 4, 2024 Butiama mkoani Mara wakati akiwasilisha salamu za Serikali kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mazishi ya Jenerali Mstaafu Musuguri. “ Katika  uhai wa kila mmoja wetu ni jambo gani mtu atakumbukwa nalo, baba huyu a...

Majaliwa Achangisha Shilingi Milioni 900 za Ujenzi wa Kanisa Kuu Lindi

  WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameendesha harambee na kuchangisha sh. milioni 928.67  za ujenzi wa kanisa kuu tarajiwa la Mt. Andrea Kagwa la Jimbo Katoliki la Lindi. Kati ya fedha hizo, sh. milioni 464.3 ni fedha taslimu na nyingine kati ya hizo zimeshawekwa benki na sh. milioni 464.37 bado ni ahadi. Awamu ya kwanza ya ujenzi huo, inatarajiwa kugharimu sh. milioni 700. Akizungumza na waumini na wadau mbalimbali waliohudhuria harambee iliyofanyika Ruangwa mjini, leo mchana (Jumamosi, Julai 27, 2024), Waziri Mkuu amewataka waliotoa ahadi wazikamilishe mapema ili kazi ya ujenzi isikwame. "Ninawashukuru sana wote mliofika na wote waliochangia ujenzi wa kanisa tarajiwa. Ninawaomba walioahidi, wakamilishe ahadi zao mapema ili kazi ianze kwani ramani ipo, mafundi wapo tayari,  wasimamizi wa ujenzi wapo," amesisitiza.  Waziri Mkuu amesema uamuzi wa Baba Askofu wa Jimbo Katoliki la Lindi, Mhashamu Askofu Wolfgang Pisa kuanza ujenzi wa kanisa kuu la jimbo hilo, ni utekelezaji ...