TANESCO: KITOVU CHA JULIUS NYERERE MW 2,115 KUIMARISHA GRIDI NA KUFANYA TANZANIA KITOVU CHA BIASHARA YA UMEME AFRICA
MKURUGENZI Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Bw. Lazaro Twange, amesema Kituo cha Uzalishaji wa Umeme cha Julius Nyerere chenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 ni hatua kubwa katika kuongeza uzalishaji wa umeme, kuimarisha Gridi ya Taifa na kuiweka Tanzania katika nafasi ya kuwa kitovu cha biashara ya umeme kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini.
Akitoa taarifa mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhusu kituo hicho wakati wa uzinduzi wake leo Agosti 22, 2026, Bw. Twange amesema mradi huo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati iliyotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya umeme nchini.
Amesema mradi huo umejengwa kwa malengo makuu matatu, ambayo ni kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini, kuimarisha Gridi ya Taifa pamoja na kuiwezesha Tanzania kushiriki kikamilifu katika biashara ya umeme na nchi za Afrika Mashariki na Kusini.
“Mradi huu umejengwa kwa malengo makubwa matatu; kwanza ni kuongeza uwezo wa kuzalisha umeme hapa nchini, pili ni kuimarisha Gridi ya Taifa kutokana na ongezeko kubwa la mahitaji ya umeme, na tatu ni kuiweka nchi yetu kama kitovu cha biashara ya umeme kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini,” amesema Twange.
Ameeleza kuwa kituo hicho kilichopo katika eneo la Mto Rufiji kimejengwa kwa kutumia mitambo yenye uwezo mkubwa wa uzalishaji, ikiwa ni pamoja na mitambo tisa ya kuzalisha umeme pamoja na transfoma 27 zinazosaidia kuongeza msongo wa umeme kutoka kilovoti 15.75 hadi kilovoti 400.
Kwa mujibu wa Twange, uwekezaji huo pia umezingatia suala la usalama wa kituo hicho, akisema TANESCO itaendelea kuimarisha mifumo ya udhibiti na kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa na kuendelea kutoa huduma kwa ufanisi.
“Kwa usalama wa taifa letu, tutaendelea kuboresha mifumo yetu ya udhibiti na kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha panakuwa na ulinzi wa nguvu na eneo hili halihatarishwi,” amesema.
Aidha, amesema TANESCO itaendelea kushirikiana na wadau wa mazingira kuhakikisha chanzo cha maji kinachotegemeza uzalishaji wa umeme katika bwawa la Julius Nyerere kinaendelea kulindwa na kuhifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Amesema uzalishaji wa umeme katika kituo hicho unategemea maji, hivyo uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji ni sehemu muhimu ya kuhakikisha uzalishaji wa umeme unaendelea kwa uendelevu.
Bw. Twange ameishukuru Serikali kwa kufanya maamuzi ya kimkakati na kuwekeza rasilimali kubwa katika mradi huo, akisema uwekezaji huo unaweka msingi wa utekelezaji wa miradi mingine mikubwa ya maendeleo itakayosaidia kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji na kutoa fursa kwa Watanzania, hususan vijana.
Amesema mradi wa Julius Nyerere unathibitisha uwezo wa Tanzania kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati pale inapoweka azma, mipango na rasilimali zinazohitajika.
“Tumetoa ujumbe kwamba tunaweza kufanya mambo yetu tukiamua, na kwamba tunaweza kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati kwa manufaa ya Taifa letu,” amesema Twange.


Comments
Post a Comment