Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema kila kitu katika Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) kimekamilika na kinafanya kazi, akieleza kuwa kukamilika kwa mradi huo ni fahari kubwa kwa Taifa na uthibitisho kwamba ndoto ya kuwa na mradi mkubwa wa kuzalisha umeme imetimia.
Rais Samia amesema hayo leo Agosti 22, 2026, wakati wa hafla ya uzinduzi wa JNHPP iliyofanyika Rufiji mkoani Pwani, ambapo amezindua Kituo cha Kuzalisha Umeme, kutembelea mitambo ya kuzalisha umeme, pamoja na kukagua tuta kuu na kituo cha kupokea na kusafirisha umeme kwenda kwenye Gridi ya Taifa.
Amesema Desemba 22, 2022 alifika katika eneo hilo kushuhudia kufungwa kwa njia ya kugeuza maji ya Mto Rufiji na kuanzishwa rasmi kwa ujazaji wa maji katika bwawa, wakati huo ujenzi wa mradi huo ukitarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka mitatu.
Kwa mujibu wa Rais Samia, kwa neema ya Mungu, bwawa hilo lilijaa ndani ya mwaka mmoja na nusu na kuanza majaribio ya uzalishaji umeme, hatua iliyowezesha mradi kuendelea kwa kasi hadi kufikia kukamilika kwake.
“Leo tumekutana tena katika eneo hili kwa ajili ya ufunguzi wa mradi huu kuwa umekamilika,” amesema Rais Samia, akieleza furaha yake ya kushuhudia matokeo ya uwekezaji mkubwa wa Taifa katika sekta ya nishati.
Amesema kukamilika kwa JNHPP ni hatua kubwa katika kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini, huku akisisitiza umuhimu wa Taifa kutumia fursa ya umeme wa uhakika katika kukuza uchumi, kuongeza shughuli za uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi.
Katika hatua nyingine, Rais Samia amewaagiza wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na viongozi wa taasisi mbalimbali kuanza mara moja maandalizi ya kukabiliana na mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha katika miezi ijayo.
Amesema taarifa za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) zinaonesha uwezekano wa Tanzania kukabiliwa na mvua kubwa, hivyo viongozi wanapaswa kuchukua hatua mapema ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.
Amewataka viongozi kuhakikisha maeneo yao yanaandaliwa na mifumo ya kukabiliana na majanga inawekwa katika hali ya utayari, ikiwemo kuimarisha miundombinu na kuchukua hatua za kuzuia athari za mvua hizo.
Rais Samia amesema maandalizi ya mapema na ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ni muhimu katika kupunguza uwezekano wa maafa na kulinda maisha, mali pamoja na miundombinu.
Pia amewataka wananchi kuwa tayari na kuchukua tahadhari, akisisitiza kuwa kila mmoja anapaswa kutimiza wajibu wake katika kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa.
Rais Samia pia amesisitiza umuhimu wa kulinda mazingira na vyanzo vya maji vinavyosaidia kujaza Bwawa la Julius Nyerere, akisema hatua hiyo ni muhimu kwa kuhakikisha uzalishaji wa umeme kupitia mradi huo unaendelea kwa uendelevu.
Amesema uendelevu wa JNHPP unategemea kwa kiasi kikubwa uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji vinavyohusiana na bwawa hilo, hivyo Watanzania wanapaswa kuchukua hatua za pamoja kuhakikisha rasilimali hizo zinalindwa kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.
Ametoa wito kwa wananchi kutambua kuwa uhifadhi wa mazingira si jukumu la Serikali pekee, bali unahitaji ushiriki wa kila mmoja katika kulinda misitu, vyanzo vya maji na maeneo yanayochangia upatikanaji wa maji katika bwawa hilo.
Aidha, Rais Samia ameiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Wizara ya Nishati, Wizara ya Maji pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, kuratibu na kusimamia kwa karibu shughuli za uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji katika maeneo yanayohusiana na JNHPP.
Amesema hatua hiyo itasaidia kulinda uzalishaji wa umeme na kuhakikisha manufaa yanayotokana na mradi huo yanaendelea kupatikana kwa Taifa kwa miaka mingi.
Rais Samia Amesema kukamilika kwa JNHPP ni mafanikio makubwa kwa Tanzania, huku akisisitiza kuwa hatua inayofuata ni kuhakikisha mradi huo unalindwa, mazingira yanahifadhiwa na umeme unaozalishwa unatumika ipasavyo kuchochea maendeleo ya Taifa.






Comments
Post a Comment