MBUNGE wa Tarime Vijijini, Mwita Waitara, amemtupia lawama Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Tarime, akidai kuwa uongozi huo uliwatelekeza wajumbe wa chama waliokuja kutoka kata mbalimbali za wilaya hiyo kwa kushindwa kuwaandalia mahitaji muhimu, ikiwemo nauli, chakula na vinywaji.
Waitara ametoa kauli hiyo mara baada ya kushiriki kongamano la Bima ya Afya pamoja na changizo la ujenzi wa bweni lililoandaliwa na Mbunge wa Viti Maalumu, Gati Chomete, akisema alilazimika kusafiri usiku kutoka Dodoma ili kushiriki shughuli hiyo kama sehemu ya kuonesha mshikamano na umoja miongoni mwa wananchi wa Mkoa wa Mara.
Amesema alifika katika shughuli hiyo kwa sababu agenda ya ujenzi wa bweni ni muhimu kwa watoto, kwani itawapa mazingira bora ya kujifunza na kujisomea, huku akisisitiza kuwa viongozi wa Mara wanapaswa kushirikiana katika shughuli zenye manufaa kwa wananchi.
“Mimi nimetoka Dodoma, nimesafiri usiku usiku kuja hapa kwenye changizo hili kwa sababu kuna agenda muhimu ya kujenga bweni kwa ajili ya watoto. Nimekuja kuonesha mshikamano na umoja wa watu wa Mara,” amesema Waitara.
Hata hivyo, Waitara ametumia nafasi hiyo kueleza kutoridhishwa kwake na namna kikao cha CCM Wilaya ya Tarime kilivyoendeshwa, akidai kuwa wajumbe kutoka kata mbalimbali waliitwa mjini Tarime kupitia utaratibu wa chama, lakini walipofika hawakupewa msaada wa mahitaji muhimu.
Amesema kikao hicho kilihusisha wajumbe zaidi ya 400 pamoja na wazee wa chama kutoka maeneo mbalimbali, ambao walifika katika ukumbi wa CMG Hotel tangu asubuhi.
Kadhalika, amesema kutokana na wajumbe hao kuitwa rasmi na chama kupitia Katibu wa Wilaya, alitarajia uongozi wa chama ungetoa ushirikiano kwa kuwaandalia chakula, vinywaji na hata nauli, badala ya kuwaelekeza kwenda kwa ofisi ya mbunge.
Waitara amedai kuwa licha ya yeye kuwa nje ya Tarime kwa majukumu ya kikazi Dodoma, taarifa ilitolewa kwamba angehusika kuwasaidia wajumbe kutoka Tarime Vijijini, jambo ambalo alisema lilimweka katika hali ngumu kutokana na idadi kubwa ya wajumbe.
“Wajumbe walialikwa na chama. Tungetegemea chama kiwape support, maana wamekuja hapa kwa mwaliko wa chama. Lakini wanaambiwa wajitegemee. Mimi nilikuwa Dodoma na nilishasema sitaweza kuwepo, lakini nilisema nitachangia kwa uwezo wangu,” amesema.
Mbunge huyo pia ameeleza kushangazwa na uamuzi wa kuwaelekeza wajumbe kutoka Tarime Vijijini kwenda kwa Katibu wa Mbunge ili kupata msaada, akidai kuwa hatua hiyo inaweza kujenga taswira kwamba yeye kama mbunge ameshindwa kuwahudumia wananchi wake.
Amesema wajumbe hao walitoka maeneo mbalimbali ya Jimbo la Tarime Vijijini, hivyo kuwahudumia wote kwa muda mfupi kunahitaji maandalizi makubwa na rasilimali za kutosha.
Waitara aliongeza kuwa anachopinga si wajumbe kupewa msaada, bali utaratibu uliotumika ambapo watu waliitwa na chama kisha jukumu la kuwahudumia likaelekezwa kwa mbunge.
“Maana yake ni nini? Anataka wale wajumbe wamtukie mbunge kwamba mbunge anaonekana kama ameshindwa kuwahudumia watu wake. Lakini yeye na wenzake wanapata nafasi ya kujisafisha. Hiki ni kitendo cha kuchonganisha watu na kuvunja mshikamano,” amesema.
Aidha, Waitara amedai kuwa changamoto hiyo imekuwepo kwa muda mrefu katika uhusiano wake na Katibu huyo wa Wilaya, akisema amekuwa akivumilia matendo anayodai yamekuwa yakilenga kumdhoofisha kisiasa.
Amedai kuwa Katibu huyo aliwahi kumtangaza kuwa hatakuwa mbunge wa Tarime Vijijini na hata kusema hamtambui, lakini licha ya tofauti hizo, yeye ameendelea kufanya kazi na wananchi pamoja na viongozi wengine.
“Amekuwa akinishughulikia sana, lakini nimevumilia. Sasa mwaka huu kuna uchaguzi, anaanza mambo haya kwa sababu anataka watu wangu waanze kuteseka ili lawama zimwangukie mbunge,” amesema.
Waitara pia amekosoa hali ya baadhi ya miundombinu ya chama wilayani Tarime, akidai kuwa baadhi ya ofisi na vibanda vya chama havijaoneshwa wazi matumizi ya mapato yake, huku akitaka kuwepo kwa uwazi na uwajibikaji katika uendeshaji wa chama.
Akizungumzia hatua za kuchukua, Waitara amesema ataandika malalamiko rasmi ndani ya chama na kutaka suala hilo lifanyiwe kazi, akisisitiza kuwa hataki tena fedha zake zitumike katika mazingira ambayo anaona hayana ushirikiano na uongozi wa chama wa wilaya.
“Nimeishatangaza. Wajumbe kutoka Tarime Vijijini wakiitwa kwenye vikao kuja Tarime mjini, kama mimi sijaalikwa au kupewa taarifa kupitia Katibu wa Mbunge, mtu yeyote asinisumbue. Kama nitakuwa na uwezo wangu, nitafanya kazi yangu moja kwa moja na wananchi na viongozi wanaoniheshimu na kutambua nafasi yangu,” amesema.
Waitara amesema licha ya tofauti hizo, ataendelea kufanya kazi na wananchi wa Tarime Vijijini, akisisitiza kuwa lengo lake ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma na maendeleo bila kuathiriwa na tofauti za kisiasa ndani ya chama.
Juhudi za kumpata katibu wa CCM wilaya ili aweze athibitishe madai haya hazikuzaa matunda baada ya simu yake ya mkononi kutopatikana na kwamba juhudi zaidi za kumtafuta zinaendelea ili aweze kuelezea madai haya.





Comments
Post a Comment