Na MASHAKA MHANDO, Tanga
MATUMIZI ya mitandao ya kijamii jijini Tanga yamechukua sura mpya ya kiuchumi, baada ya vijana zaidi ya 150 kunufaika na mradi maalum wa ujuzi wa kidijitali uliowatoa mitaani na kuwafanya kuwa watengeneza maudhui (Content Creators) wanaojitegemea na kujingizia kipato.
Mradi huo umewasaidia vijana kuachana na dhana potofu kuwa mitandao ya kijamii haina faida, na badala yake wamepewa ujuzi wa kuandaa maudhui, kupiga picha, na kuhariri kazi zenye viwango vinavyokidhi masoko ya mtandaoni.
Miongoni mwa shuhuda za kusisimua za mradi huu ni ya Peter Msuya, kijana ambaye awali alikuwa fundi stadi wa kutengeneza vitanda na makochi (Sofa). Peter anasema maisha yake yamebadilika kabisa baada ya kujiunga na mafunzo hayo ya kidijitali.
"Nashukuru sana mafunzo niliyopata. Leo hii ukurasa wangu unafuatiliwa na watu milioni mbili! Kama siyo mradi wa 'Tanga Yetu', saa hii ningekuwa nagombana na wateja ambao sijawatengenezea vitanda vyao kwa wakati. Sasa naweza kuandaa maudhui, kupiga picha zenye viwango, na kuhariri kazi zenye ubora," alijigamba Peter, akibainisha kuwa mradi huo umefuta dhana ya kuwa vijana wa Tanga ni wavivu.
Naye Jumaa Said, kijana aliyejikita kwenye utengenezaji wa maudhui ya changamoto za mahusiano na maisha (Interviews & Challenges), amesema mradi huo ulimkuta akiwa na ndoto kubwa asiyojua namna ya kuitimiza.
"Nilikuwa sijui ndoto zangu nani ataziunga mkono kwa sababu sikuwa najua chochote kile. Lakini kupitia mkufunzi wetu Daniel Kileo wa Swahili Digital, nilijifunza kuandaa maudhui, kuhariri, na kupiga picha. Nikaamua kushika hili eneo kwa sababu ndilo litanifanya nifike mbali," alisema Jumaa.
Jumaa ametumia fursa hiyo kuonya vijana wenzake dhidi ya matumizi mabaya ya mitandao. "Nawaasa vijana wasitumie mitandao kutukana Serikali, kuchafua watu, au kusambaza maudhui ya watu wengine bila kujua madhara yake. Watengeneze maudhui yao yenye faida kwa jamii na wawe na msimamo (endelevu) kwenye kile wanachokifanya," alishauri.
Akifafanua kuhusu chimbuko la mafanikio hayo, Mratibu wa Mradi wa Kidijitali, Yusuph Yusuph, amesema mradi huo unajulikana kama "Digital Skills for Sustainable Wealth Development" ulianza rasmi Juni 2025.
Mradi huu unatekelezwa na taasisi ya Swahili Digital, ukisimamiwa na programu ya Tanga Yetu chini ya Halmashauri ya Jiji la Tanga, kwa ufadhili wa Fondation Botnar kupitia shirika la Innovex.
Yusuph ameeleza kuwa mradi ulianza kwa kukusanya vijana 300, ambapo baada ya mchujo walibaki vijana 250 walioanza mafunzo rasmi na kwamba hadi sasa, vijana 150 wamehitimu na wanafanya vizuri mitaani kupitia shughuli mbalimbali za kidijitali.
"Vijana hawapati ujuzi pekee; wanatumia ujuzi huo kupata ajira, kuanzisha biashara, kujipatia kipato, na muhimu zaidi, kufungua fursa kwa vijana wengine," alihitimisha Yusuph.



Comments
Post a Comment