Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Bw. Mohamed Salum, amesema kukamilika kwa ukarabati wa meli ya MV Liemba kutaimarisha huduma za usafiri wa majini, kuchochea biashara na kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Mkoa wa Kigoma na ukanda mzima wa Ziwa Tanganyika.
Bw. Salum amesema hayo leo, tarehe 23 Juni, 2026 alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ukarabati wa meli hiyo katika Bandari ya Kigoma, ikiwa ni sehemu ya shughuli za Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani humo.
Amesema wananchi wanaoishi katika maeneo yanayozunguka Ziwa Tanganyika wanategemea kwa kiwango kikubwa usafiri wa majini kwa shughuli za biashara, usafirishaji wa bidhaa na huduma za kijamii, hivyo kukamilika kwa MV Liemba kutaboresha huduma hizo na kuongeza ufanisi wa usafiri salama na wa uhakika.
"MV Liemba ni meli yenye umuhimu mkubwa kwa wananchi wa ukanda wa Ziwa Tanganyika. Kukamilika kwake kutaimarisha usafiri salama, kurahisisha biashara, kuunganisha jamii na kufungua fursa zaidi za maendeleo ya kiuchumi," amesema Bw. Salum.
Ameongeza kuwa Mkoa wa Kigoma utanufaika zaidi kupitia kuongezeka kwa shughuli za biashara, usafirishaji wa abiria na mizigo pamoja na fursa nyingine za kiuchumi zitakazotokana na kurejea kwa huduma za meli hiyo.
Aidha, amesema uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali katika ukarabati wa MV Liemba unaonyesha dhamira ya kuimarisha sekta ya usafiri wa majini, kuongeza usalama wa usafiri na kuendeleza uchumi wa buluu nchini.
Ziara hiyo ya Mkurugenzi Mkuu wa TASAC ni sehemu ya shughuli za Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma, yanayolenga kutambua mchango wa mabaharia na wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika maendeleo ya Taifa, pamoja na kuhamasisha usalama, ustawi na maendeleo ya sekta hiyo.







Comments
Post a Comment