MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ameitaka Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuimarisha usimamizi wa vyama vya ushirika nchini ili kuhakikisha vinaendeshwa kwa uwazi, uwajibikaji na uadilifu, akisisitiza kuwa ushirika wenye misingi hiyo ndiyo nguzo muhimu ya kukuza uchumi jumuishi na kuvutia uwekezaji.
Dkt. Nchimbi ametoa kauli hiyo leo katika Siku Maalum ya Ushirika, iliyofanyika ndani ya Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane 2026 kwenye Viwanja vya John Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma, ambapo pia amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha sekta ya ushirika ili iwe kichocheo cha maendeleo ya kilimo na uchumi wa Taifa.
Amesema Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) linapaswa kuendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa vyama vya ushirika ili kudhibiti ubadhirifu wa rasilimali, kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha na kuongeza uwazi katika uendeshaji wa vyama hivyo.
"Ushirika wenye uadilifu unajenga imani kwa wanachama na wadau, unaongeza uwajibikaji na kuvutia uwekezaji unaochochea maendeleo ya sekta hii. Kuimarika kwa ushirika kunategemea uaminifu, uwajibikaji na uadilifu wa viongozi, watendaji na wanachama wake," amesema Makamu wa Rais.
Aidha, ametoa wito kwa taasisi za Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kushirikiana na Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika utekelezaji wa kampeni ya "Linda Ushirika, Chagua Uadilifu," inayolenga kutokomeza vitendo vya rushwa, ubadhirifu na uhalifu mwingine unaodhoofisha maendeleo ya vyama vya ushirika.
Makamu wa Rais pia ameielekeza Wizara ya Kilimo kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuhakikisha sekta hiyo inakwenda sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuijenga kuwa ya kisasa, yenye ushindani na inayotumia fursa za biashara kuongeza kipato cha wanachama na kuchangia ukuaji wa uchumi wa viwanda.
Vilevile, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida za kujiunga na vyama vya ushirika ili kuongeza ushiriki wao katika shughuli za uzalishaji na biashara, sambamba na kufanikisha malengo ya Serikali ya kupanua wigo wa ushirika nchini.
Akizungumzia sekta ya kilimo, Dkt. Nchimbi amesema Serikali itaendelea kuboresha huduma kwa wakulima kupitia upatikanaji wa pembejeo, huduma za ugani na kuimarisha mpango wa ruzuku ya mbolea, hatua ambazo zinalenga kuongeza matumizi ya mbolea, kuinua tija mashambani na kuongeza uzalishaji wa mazao kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi.
Baada ya shughuli hiyo, Makamu wa Rais alishiriki maadhimisho ya miaka 10 ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), ambapo aliipongeza taasisi hiyo kwa mchango wake mkubwa katika kubuni teknolojia na kufanya tafiti zilizoleta mageuzi makubwa katika sekta ya kilimo kwa kipindi cha muongo mmoja uliopita.
Amesema mafanikio ya TARI yanaonesha umuhimu wa kuwekeza katika tafiti, sayansi na ubunifu ili kupata suluhisho la changamoto zinazowakabili wakulima na kuongeza ushindani wa mazao ya Tanzania katika masoko ya kimataifa.
"Dira ya Taifa 2050 inatupa wajibu wa kuhakikisha tafiti na ubunifu vinatoa matokeo yanayoonekana. Tunahitaji teknolojia zinazoongeza tija, thamani ya mazao na ushindani wa sekta ya kilimo ili kujenga uchumi imara na endelevu," amesema.
Makamu wa Rais ameongeza kuwa historia inaonesha kuwa mataifa yaliyopiga hatua kubwa kiuchumi yalifanikiwa kwa kuwekeza katika elimu, sayansi, teknolojia na ubunifu, akieleza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa taasisi za utafiti ili ziendelee kuzalisha maarifa yanayochochea maendeleo ya Taifa.
Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane 2026 yanaendelea katika Viwanja vya John Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma, yakibeba kaulimbiu isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira 2050," inayohamasisha matumizi ya teknolojia, kuongeza uzalishaji na kuimarisha ushindani wa sekta ya kilimo katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa.





Comments
Post a Comment