Jiji la Mwanza limepiga hatua nyingine katika jitihada za kutatua changamoto ya muda mrefu ya upatikanaji wa maji baada ya kusainiwa kwa mkataba wa mkopo wenye masharti nafuu wa Shilingi bilioni 39 kwa ajili ya utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Chanzo cha Maji Butimba.
Mkataba huo uliosainiwa jijini Mwanza baina ya Umoja wa Ulaya (EU) na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD), ni sehemu ya uwekezaji mkubwa unaolenga kuongeza uzalishaji wa maji, kuimarisha miundombinu ya usambazaji na kuhakikisha wakazi wa Jiji la Mwanza wanapata huduma ya maji yenye uhakika.
Kwa sasa, Jiji la Mwanza linategemea vyanzo viwili vikuu vya maji vya Butimba na Capri Point ambavyo kwa pamoja vina uwezo wa kuzalisha takribani lita za ujazo milioni 138 za maji kwa siku.
Hata hivyo, mahitaji ya maji kwa wakazi wa jiji hilo yamefikia takribani lita za ujazo milioni 188 kwa siku, hali inayosababisha kuwepo kwa nakisi ya takribani lita za ujazo milioni 50 za maji kila siku.
Utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Chanzo cha Maji Butimba unatarajiwa kuwa suluhisho muhimu katika kupunguza pengo hilo, ambapo baada ya kukamilika utaongeza uwezo wa uzalishaji wa maji hadi kufikia takribani lita za ujazo milioni 170 kwa siku.
Mradi huo ni sehemu ya programu ya LV WATSAN na unatarajiwa kugharimu zaidi ya Shilingi bilioni 600. Katika utekelezaji wake, Serikali ya Tanzania itanufaika na mkopo wa Euro milioni 190 kutoka Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB) pamoja na washirika wengine wa maendeleo, huku pia ikipata mkopo wenye masharti nafuu wa Euro milioni 12.93 kutoka Umoja wa Ulaya.
Fedha hizo zinalenga kuongeza uwezo wa miundombinu ya maji na usafi wa mazingira, sambamba na kukidhi mahitaji yanayoongezeka kutokana na kasi ya ukuaji wa Jiji la Mwanza.
Akizungumza katika hafla ya kusainiwa kwa mkataba huo, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Christine Grau, amesema uwekezaji huo ni sehemu ya ushirikiano wa muda mrefu wa zaidi ya miaka 50 kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya.
Amesema kupitia mkakati wa Global Gateway, Umoja wa Ulaya pamoja na nchi wanachama wake wameendelea kuiunga mkono Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo sekta ya maji, nishati safi, mabadiliko ya kidijitali na maendeleo ya kilimo.
"Mwaka jana tuliadhimisha miaka 50 ya ushirikiano kati ya Umoja wa Ulaya na Tanzania. Leo tunaendelea kujenga ushirikiano huo kupitia uwekezaji katika sekta ya maji na usafi wa mazingira kwa manufaa ya wananchi wa Mwanza na Tanzania kwa ujumla."
Balozi Grau amesema Mwanza ina nafasi muhimu kiuchumi kutokana na kuwa lango la Jumuiya ya Afrika Mashariki, jambo lililofanya jiji hilo kuwa miongoni mwa maeneo yanayonufaika na ushirikiano kati ya Tanzania na Team Europe.
Amesema Umoja wa Ulaya umeendelea kuona matokeo ya miradi inayofadhiliwa mkoani Mwanza, ikiwemo mradi wa SASA, huku sekta ya maji ikiendelea kuwa eneo la kipaumbele.
Aidha, ameishukuru Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA), Wizara ya Maji na viongozi wa Mkoa wa Mwanza kwa ushirikiano waliouonyesha katika maandalizi na utekelezaji wa miradi hiyo.Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika Mashariki wa Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD), amesema uwekezaji huo unaonyesha dhamira ya washirika wa maendeleo kuendelea kuunga mkono Tanzania katika kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.
"Uwekezaji katika sekta ya maji una mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii na uchumi. Kupatikana kwa maji ya uhakika kunasaidia afya, biashara na maendeleo ya wananchi kwa ujumla."
Naye Meneja wa Programu za Miundombinu kutoka Ofisi ya Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Mhandisi Ally Chande, amesema Umoja wa Ulaya umekuwa mshirika wa karibu wa Mwanza katika sekta ya maji kwa zaidi ya miaka 20.
Amesema mbali na utekelezaji wa Butimba Phase Two, Umoja wa Ulaya unaendelea kutathmini uwezekano wa kusaidia maandalizi ya ujenzi wa chanzo kipya cha maji katika eneo la Kabangaja, kitakacholenga kuongeza upatikanaji wa maji katika maeneo ya kaskazini mwa Jiji la Mwanza.
"Kwa zaidi ya miaka 20 tumekuwa tukishirikiana na Tanzania katika miradi ya maji Mwanza. Tunaendelea kuangalia hatua zinazofuata ili kuhakikisha huduma ya maji inaendana na ukuaji wa jiji."
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira kutoka Wizara ya Maji, Mhandisi Charles Mwafwili, amesema mradi huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kutatua changamoto ya maji katika Mwanza.
"Mradi huu utaongeza uzalishaji wa maji, kupunguza pengo lililopo kati ya mahitaji na uzalishaji wa sasa, na kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi."
Awamu ya Pili ya Mradi wa Chanzo cha Maji Butimba inatarajiwa kuanza kutekelezwa katika kipindi kifupi kijacho na kukamilika ndani ya miezi 12 hadi 24.
Kwa wakazi wa Mwanza ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji, mradi huu unatajwa kuwa hatua muhimu kuelekea kuhakikisha huduma ya maji inakwenda sambamba na kasi ya ukuaji wa jiji hilo.







Comments
Post a Comment