BODI ya Stakabadhi za Ghala (WRRB) imesema imejipanga kupanua wigo wa mfumo wa stakabadhi za ghala kwa kusajili mazao mapya yakiwemo mazao ya viungo na mifugo, hatua inayotarajiwa kuongeza fursa za masoko, kuwawezesha wakulima kupata huduma za kifedha na kuimarisha biashara ya mazao nchini.
Akizungumza leo jul 31,2026 jijini Dodoma wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Bodi kwa mwaka wa fedha 2025/2026 pamoja na mwelekeo wa mwaka wa fedha 2026/2027, Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo, Asangye Bangu, amesema taasisi hiyo imepata uzoefu wa kutosha katika usimamizi wa mfumo wa stakabadhi za ghala na sasa imejielekeza kuongeza mazao yatakayohudumiwa ili kuwafikia wazalishaji wengi zaidi.
Amesema katika hatua za awali, Bodi inalenga kuingiza mazao ya viungo kama iliki, tangawizi, kitunguu saumu na pilipili manga (black pepper), huku ikiendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi zinazoratibu maendeleo ya mazao hayo ili kuhakikisha yanaingizwa rasmi kwenye mfumo wa stakabadhi za ghala.
"Tumepata uzoefu wa kutosha katika usimamizi wa mfumo wa stakabadhi za ghala. Sasa tunapanua wigo kwa kuingiza mazao ya viungo kama iliki, tangawizi, kitunguu saumu na pilipili manga. Tunashirikiana kwa karibu na taasisi husika na matarajio yetu ni kwamba ifikapo Julai mwaka ujao mazao mengi zaidi yatakuwa yameanza kuhudumiwa kupitia mfumo huu," amesema Bangu.
Amebainisha kuwa hadi sasa Bodi imesajili mazao 18 yakiwemo mahindi, mpunga, kahawa, korosho, karanga na asali, huku huduma za mfumo wa stakabadhi za ghala zikipanuka na kufikia mikoa 23 nchini, ikiwemo Dodoma na Morogoro. Amesema hatua hiyo imeongeza ushiriki wa wakulima, vyama vya ushirika na wafanyabiashara katika mfumo huo na kusaidia kuboresha biashara ya mazao.
Mbali na kupanua usajili wa mazao, Bangu amesema Bodi imeanza kutekeleza mkakati wa kuwaunganisha wakulima na taasisi za fedha ili kuwawezesha kupata mikopo kwa kutumia stakabadhi za mazao yaliyohifadhiwa kwenye maghala yaliyosajiliwa.
Amesema kupitia utaratibu huo, mkulima hatahitajika kuuza mazao yake kwa haraka kutokana na uhitaji wa fedha, bali ataweza kuhifadhi mazao yake, kupata stakabadhi na kuitumia kama dhamana ya kupata sehemu ya fedha kutoka benki wakati akisubiri mazao kuuzwa kwa bei nzuri.
"Mkulima akiingiza mazao yake kwenye ghala lililosajiliwa atapatiwa stakabadhi ambayo itamwezesha kwenda benki kupata sehemu ya fedha kwa ajili ya kujikimu wakati akisubiri mnada wa mazao yake. Hii itawaondolea wakulima shinikizo la kuuza mazao kwa bei ya chini kwa sababu ya mahitaji ya fedha za haraka," amesema.
Ameongeza kuwa utekelezaji wa mpango huo umeanza kwa majaribio mkoani Rukwa na baada ya kukamilika utaongezwa katika maeneo mengine makubwa yanayozalisha mahindi, mpunga na mazao mengine ya kimkakati.
Kwa mujibu wa Bangu, katika mwaka wa fedha 2026/2027 Bodi itaendelea kuboresha mifumo ya kidijitali, kupanua huduma za stakabadhi za ghala katika maeneo mapya na kuongeza usajili wa mazao ili kuwapa wakulima na wafanyabiashara fursa zaidi za kupata masoko yenye ushindani, huduma za kifedha na kuongeza thamani ya mazao yao.





Comments
Post a Comment