Na Mwandishi wetu Jovina Massano.
Mamlaka ya Usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA) Kituo Cha Mwanza imekutana na waganga wa tiba za asili na mbadala kwa kuwapatia elimu ya uhifadhi ikiwemo umiliki nyara wanazotumia katika shughuli zao.
Akitoa elimu hiyo mbele ya Katibu Mtendaji wa Umoja wa Machifu Tanzania ambae pia ni Mtemi Nyamilonda wa tatu Harun Mkomangwa Wilayani Ilemela mkoani humo mhifadhi wa wanyamapori kutoka TAWA Bw. Omary Mhando amewafafanulia umuhimu wa kutunza maliasili na kufuata taratibu za umiliki wa nyara kwa mujibu wa sheria za uhifadhi.
Hakusita kuwambusha namna Serikali ya awamu ya sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan inavyoendelea kuwajali na kuwasikiliza wananchi wake na kutambua umuhimu wao na kuhakikisha inawajengea uelewa mpana kwa kuweka utaratibu wa kutoa elimu ya uhifadhi ambayo itawezesha kuongeza wigo mpana wa kulinda maliasili kwa uhifadhi endelevu wenye misingi thabiti kwa vizazi hata vijavyo.
Sanjari na hayo amewaeleza pia umuhimu wa kuzingatia pamoja na kufuata taratibu zilizowekwa na Mamlaka kwa kuwapa amani za umiliki wa maliasili (nyara) ili kuweza kufanya kazi zao bila hofu yeyote.
" Utunzaji wa maliasili zetu ni muhimu Sana kwa kuwa waganga wa tiba asili na mbadala wengi wanategemea baadhi ya vitendea kazi vinavyotokana na maliasili hizo katika shughuli mbalimbali "amesema Mhando.
Kwa Upande wake Katibu Mtendaji wa Umoja wa Machifu Tanzania Mtemi Harun Mkomangwa ameipongeza Serikali na Mamlaka ya Usimamizi wa wanyamapori Tanzania(TAWA) kwa kuwapatia elimu ya uhifadhi ambayo itawasaidia wakati wa uteketezaji wa majukumu yao.
Ameongeza kuwa elimu hii imewafungua waganga kwa kiwango Cha juu na kuwaondoa hofu na imewapa uelewa mpana wa kulinda maliasili kwa mustakabali wa Taifa na kumiliki nyara kwa kufuata miongozo ya kisheria.
Mtemi Harun ameiomba TAWA kuyafikia makundi yote katika jamii hasa makundi ambayo hutumia dhana zitokanazo na mazao ya maliasili kwa kuwa hutumiwa katika shughuli zao za mila na desturi bila kusahau ngoma za asili.
Ameainisha makundi hayo kuwa ni pamoja na machifu wote,waganga wa tiba asili na mbadala wakiwemo manju wa ngoma za asili.
Washiriki wametoka katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga,Geita,Simiyu,Kagera na Mara.



Comments
Post a Comment