Wananchi wa Kijiji cha Kaitambunzi, Kata ya Isingiro wilayani Kyerwa, wameiomba Serikali kuchunguza utaratibu unaotumiwa na baadhi ya maafisa wa Uhamiaji wakati wa operesheni za usiku za kusaka wahamiaji haramu, wakidai zimekuwa zikisababisha hofu hata kwa raia wasiokuwa na makosa.
Kero hiyo iliwasilishwa katika mkutano wa hadhara wa Mbunge wa Jimbo la Kyerwa, Khalid Nsekela, ambapo wananchi walisema wanaunga mkono juhudi za Serikali za kudhibiti uhamiaji haramu, lakini wakasisitiza operesheni zifanyike kwa kuzingatia sheria, taratibu na haki za wananchi.
Alistidia Mbatina ni mkazi wa kijiji hicho amesema kuwa licha ya kuunga mkono juhudi za Serikali za kudhibiti uhamiaji haramu, wanahitaji operesheni hizo kufanyika kwa kuzingatia sheria, taratibu na haki za wananchi ili kuepusha taharuki na hofu isiyo ya lazima ambayo inawakabili kwa sasa.
"Operesheni zinazofanyika nyakati za usiku wa manane zimekuwa zikitutia hofu,wanakuja watu wanakamata watu uwe muhamijai haramu au mzawa kwakweli siyo salama tunaomba Serikali iingilie kati suala hili na mbunge utasaidia kuongea nao wafuate taratibu""ameeleza Mbatina.
Akijibu malalamiko hayo, Nsekela amesema tayari amewasiliana na mamlaka husika, akisisitiza kuwa hakuna anayepinga mapambano dhidi ya uhamiaji haramu, lakini utekelezaji wake unapaswa kuzingatia sheria na kujenga imani kati ya wananchi na vyombo vya dola.
Nsekela amesisitiza kuwa usalama wa mipaka ni muhimu, lakini pia ni lazima wananchi wahudumiwe kwa njia inayojenga imani na ushirikiano kati yao na vyombo vya dola huku akiwaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola, ikiwemo kutoa taarifa wanapoona wahamiaji haramu na watu wanaojihusisha na vitendo vya uvunjifu amani ili vichukuliwe hatu kwa mujibu wa sheria.
Katika hatua nyingine, akiwa Kata ya Mulongo, mbunge huyo aliagiza viongozi wanaosimamia ukusanyaji wa ushuru katika Soko la Ndizi Mulongo kuhakikisha tozo zote zinazingatia sheria na taratibu, kufuatia malalamiko ya wakulima na wafanyabiashara kuhusu ushuru unaodaiwa kuwa si wa haki.
Ziara za Nsekela zinaendelea katika maeneo mbalimbali ya Jimbo la Kyerwa kwa lengo la kusikiliza kero za wananchi na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za maendeleo.







Comments
Post a Comment