Na Angela Sebastian ;Muleba
MSEMAJI wa Klabu ya Simba, Ahmed Ally
amemtaka mwaandaaji wa Mashindano ya Mwijage Cup ambayo yanahusisha timu 20 za ndondo kutoka katika Tarafa ya Kamachumu Wilayani Muleba mkoani Kagera, kuyafanya kwa malengo ya muda mrefu na yawe yenye kuibua vipaji kuliko kusubiri muda wa kuomba kura au jambo fulani linalohusu maslahi binafsi.
Ally ametoa rai hiyo jana wakati akizindua mashindano hayo katika uwanja wa mpira wa polisi Kamachumu ulioko katika kata ya Kamachumu ambayo yanalenga kuwasaidia vijana kujengewa uwezo wa kucheza mpira wenye viwango vya kimataifa,kuinua vipaji na kutengeneza vipaji vipya kwenye mpira wa miguu kutoka ngazi za chini watakaokwenda kucheza kwenye timu kubwa hapo baadaye.
"Mwanzilishi na mdhamini wa mashindano haya (Paul Mwijage) jamii mnapaswa kumuunga mkono ili aendeelee kuwafanyia mema wana michezo hasa wakazi wa Tarafa Kamachumu kwani malengo yake ni kuwaunganisha nyinyi hususani vijana kupitia michezo hivyo yawe endelevu na siyo kama wafanyavyo baadhi ya watu mfano wakati wa uchaguzi watu wanaanzisha ligi alafu wasipofanikiwa ndo inakuwa mwisho wa mashindano hayo"amesema Ally.
Amesema amefurahi kufika Kamachumu na kukutana wanachama wa Simba na wapenda michezo,"nimeona kuna mwamko mkubwa wa michezo hasa mpira wa miguu, tumuunge mkono Mwanzilishi wa mashindano haya ambaye amewafanya vijana kuonekana kupitia vipaji vyao vya mpira" amesema.
Pia amesisitiza kualika watu wenye maamuzi katika ligi hiyo wakati ikiendelea ili wafanye usajili wa vijana kutoka maeneo mbalimbali pia kushirikisha wataalamu ambao wamesomea mpira ili waweze kupata wachezaji kutoka ngazi ya chini.
"Haya mashindano siyo ya kubeza yanaibua vipaji ambavyo sisi tulioko huku juu hatuwezi kuvigundua mfano sisi Simba tuliwahi kupata mchezaji mzuri aitwaye Seleman Mwalimu kutoka kwenye timu ndogo ya Hai kule mkoani Kilimanjaro hivyo,huku chini kuna vipaji"amesema
Paul Mwijage ambaye ni mdhamini na muandaaji wa mashindano hayo amesema, lengo la mashindano hayo ni kukuza vipaji vya vijana ambao wanateketea kwa ulevi,madawa ya kulevya,yatima wasio na msaada hivyo kupitia mashindano ya mpira wa miguu wataweza kuyatumia kama fursa kujiunua katika masuala mbalimbali kwa kutumia vipaji vyao.
"Lengo la mimi kuja kuwekeza nyumbani kwa kuanzisha ligi hii ni kutaka kukuza vipaji vya michezo kwa vijana wengi wanaopoteza matumaini katika soka, tumelenga Kusaidia kukuza soka la Tarafa Kamachumu,Wilaya ya Muleba,Mkoa na Taifa ndiyo maana tumemleta Msemaji wa Simba Ahmed Ally ili na yeye aone kuwa hata vijijini kuna vipaji vya mpira kutoka kwa Vijana wetu" amesema Mwijage.
Mwijage ameeleza kuwa, timu 20 kutoka tarafa ya Kamachumu zitashiriki katika ligi hiyo ambayo itaendelea kwa kipindi cha miaka 10 huku akiwashauri vijana wenzake kurudi kuwekeza nyumbani.
Naye Afisa michezo na utamaduni wa Halmashauri ya Wilaya ya Muleba Denis Joseph amesema wao kama Serikali ni yao ni kuwaunga mkono wale wote wenye nia ya kuanzisha ligi kama hizo waje waibue vipaji na wasikate tamaa lengo ni kuibua na kupata wachezaji wazuri ambao ni alama ya kuitangaza Wilaya hiyo ndani na nje ya nchi.






Comments
Post a Comment