WIZARA YA MAENDELEO YA JAMII YAIPA KIPAUMBELE AJENDA YA MALEZI NA USTAWI WA WATOTO KATIKA BAJETI YA 2026/27
Akiwasilisha bajeti ya wizara hiyo bungeni jijini Dodoma, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema Serikali imeandaa vipaumbele saba vya kimkakati vitakavyoongoza utekelezaji wa mipango yake, huku ujenzi wa mtaji watu ukichukua nafasi ya juu katika safari ya kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Amesema pamoja na kuendelea kuimarisha uchumi na miundombinu, Serikali inaona umuhimu wa kuwekeza kwa nguvu katika watoto wa leo kwa kuwa ndio watakaobeba hatma ya Tanzania katika miaka ijayo kama viongozi, wataalamu na nguvu kazi ya Taifa.
Dk. Gwajima ameeleza kuwa mabadiliko ya kijamii yanayoendelea kushuhudiwa yameibua changamoto mbalimbali zinazohitaji hatua za haraka, ikiwemo kuporomoka kwa maadili, ongezeko la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, matumizi ya dawa za kulevya, mimba za utotoni, matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii pamoja na migogoro ya kifamilia.
Kutokana na hali hiyo, Serikali imebainisha maeneo sita ya kipaumbele yatakayosaidia kuimarisha malezi na ustawi wa watoto nchini. Maeneo hayo ni pamoja na kuimarisha taasisi ya familia, kujenga mfumo imara wa maadili ya Taifa, kuimarisha mifumo ya ulinzi wa mtoto, kuwekeza katika makuzi ya awali ya mtoto, kulinda afya ya akili ya watoto na kujenga jamii inayoshiriki kikamilifu katika malezi na ustawi wa mtoto.
Amesisitiza kuwa uwekezaji katika mtoto ni uwekezaji katika mustakabali wa Taifa, akieleza kuwa mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yatategemea kwa kiwango kikubwa namna Taifa linavyowalea na kuwaandaa watoto wa sasa kuwa raia wenye maadili, maarifa na uzalendo.
"Malezi bora ya mtoto wa leo ndiyo msingi wa amani, usalama, uchumi imara na maendeleo ya Tanzania ya kesho. Tusipowekeza kwa watoto wetu sasa, tutalazimika kutumia gharama kubwa kurekebisha changamoto za kijamii baadaye," alisema Dk. Gwajima.
Katika mwaka wa fedha 2026/27, wizara pia itaendelea kutekeleza programu mbalimbali za kuimarisha ustawi wa vijana balehe, kukabiliana na ukatili wa mtandaoni dhidi ya watoto, kuboresha huduma za ustawi wa jamii kwa makundi maalum na kuongeza fursa za kiuchumi kwa wanawake, vijana, wazee na watu wenye ulemavu.
Aidha, Serikali itaendelea kuhimiza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi, kuimarisha mifumo ya bajeti zinazozingatia usawa wa kijinsia, kulinda haki za wajane na kuwashirikisha wanaume katika juhudi za kutokomeza ukatili wa kijinsia na kujenga jamii yenye usawa na mshikamano.
Wizara imeeleza kuwa mafanikio ya malengo hayo yatategemea pia ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, mashirika yasiyo ya kiserikali na washirika wa maendeleo, ambao wataendelea kushirikishwa katika kuimarisha huduma za kijamii na ustawi wa wananchi kuelekea Tanzania ya mwaka 2050.


Comments
Post a Comment