UONGOZI WA JUU IPU WAKUTANA NA SPIKA ZUNGU NEW YORK, WAPOKEA HAKIKISHO LA UENYEJI WA MKUTANO WA 153 JIJINI ARUSHA
Na Prosper Makene
New York, Marekani– Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Musa Azzan Zungu, ameuhakikishia Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) kuwa Tanzania imejipanga kikamilifu kuandaa Mkutano wa 153 wa IPU utakaofanyika Oktoba 2026 jijini Arusha.
Mhe. Zungu ametoa hakikisho hilo wakati wa kikao na Rais wa IPU, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Mbunge, pamoja na Katibu Mkuu wa IPU, Balozi Anda Filip jijini New York, Marekani.
Kikao hicho kililenga kupitia hali ya maandalizi, mipango ya kilojisti na uhakika wa utayari kabla ya mkutano huo mkubwa wa kibunge duniani.
Spika ameeleza kuridhishwa na kazi ya Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi inayoratibu tukio hilo. Amesema mipango yote ya kilojisti, kiprotocol na usalama inaendelea kama ilivyopangwa, na Tanzania imejitolea kutoa ukaribisho wa kiwango cha kimataifa.
Mhe. Zungu amesisitiza kuwa kuandaa mkutano huo ni jambo la fahari kwa Taifa na ni fursa muhimu ya kuimarisha nafasi ya Tanzania katika diplomasia ya kibunge duniani.
Ameongeza kuwa Mkutano huo utakuwa jukwaa muhimu la majadiliano, ushirikiano na utafutaji wa masuluhisho ya changamoto zinazolikabili dunia leo. Tanzania inajivunia kuwakaribisha Maspika, Wabunge na wajumbe kutoka pande mbalimbali za dunia jijini Arusha, mji unaojulikana kwa amani na diplomasia.
Katibu Mkuu wa IPU, Balozi Anda Filip, naye amepongeza Tanzania kwa maendeleo yaliyopatikana katika maandalizi. Amethibitisha kuendelea kwa ushirikiano na msaada wa Sekretarieti ya IPU kwa Bunge la Tanzania ili kuhakikisha mafanikio ya Mkutano huo.
Mkutano wa 153 wa IPU unatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki zaidi ya 1,500 wakiwemo Waspika wa Bunge, Wabunge na wajumbe kutoka mabunge 180 wanachama wa IPU na wanachama 15 washirika.
Ajenda ya Mkutano itagusa masuala mbalimbali ya kimataifa. Miongoni mwa masuala hayo ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, amani na usalama, utawala wa teknolojia, haki za binadamu, usawa wa kijinsia, na jukumu la mabunge katika kuharakisha utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu. Mpango wa mkutano utajumuisha mijadala ya wazi, vikao vya kamati na mikutano ya pande mbili baina ya ujumbe.
Arusha, inayofahamika kama 'Geneva ya Afrika' imechaguliwa kuwa mwenyeji kutokana na sifa yake ya kimataifa kama kituo cha diplomasia, amani na mikutano ya kimataifa.
Mji huo una historia ya kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa ikiwemo vikao vya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Rwanda na mikutano mbalimbali ya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika.
Serikali ya Tanzania imesema Mkutano huo utaleta manufaa makubwa kwa mji wa Arusha na kwa Taifa kwa ujumla. Manufaa yanayotarajiwa ni pamoja na kukuza utalii, huduma za ukaribishaji na ubadilishanaji wa kitamaduni. Pia tukio hili litaonesha miundombinu ya Tanzania na uwezo wake wa kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa.

Comments
Post a Comment