Na Mwanamkuu Mwandoro,Mkinga.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato kupitia usimamizi makini wa forodha ili kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya ndani, kukuza biashara halali na kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Mhe. Waziri amesema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Kituo cha Forodha cha Horohoro kilichopo Wilaya ya Mkinga, mkoani Tanga, ambapo alipata fursa ya kutathmini utendaji wa kituo hicho na kujionea mafanikio yaliyopatikana katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.
Alisema mafanikio yaliyofikiwa na Kituo cha Forodha cha Horohoro yanaonesha kuwa juhudi za Serikali za kuimarisha usimamizi wa forodha zinaendelea kuzaa matunda, huku mapato yanayokusanywa yakitoa mchango mkubwa katika kugharamia miradi ya maendeleo na kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi.
"Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato kupitia usimamizi makini wa forodha. Mapato haya ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma muhimu kwa wananchi, hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha kila stahiki ya Serikali inakusanywa kwa ufanisi," alisema Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar.
Katika ziara hiyo, Waziri huyo aliipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kupitia Kituo cha Forodha cha Horohoro kwa kuvuka lengo la makusanyo ya mapato kwa asilimia nane, baada ya kukusanya Shilingi Bilioni 125 dhidi ya lengo la Shilingi Bilioni 115 katika kipindi husika.
"Kiwango cha mapato ambacho mmekikusanya kimepindukia lengo. Tumekusanya Shilingi Bilioni 125 dhidi ya lengo la Bilioni 115 na hivyo kuvuka lengo kwa asilimia nane. Hii ni kazi nzuri inayostahili pongezi, na kila mtumishi aliyeshiriki ametoa mchango mkubwa kufanikisha matokeo haya," alisema.
Aidha, Mhe. Waziri alivipongeza vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na taasisi nyingine zinazoshirikiana katika usimamizi wa mpaka wa Horohoro kwa mchango wao katika kudhibiti biashara haramu na ukwepaji wa mapato ya Serikali.
"Mafanikio haya ni matokeo ya ushirikiano mzuri kati ya TRA, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na taasisi nyingine zinazotekeleza majukumu katika mpaka huu. Ushirikiano huu umeongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato na unapaswa kuendelezwa," alisisitiza.
Vilevile, aliwataka Maafisa wa Forodha kuendelea kusimamia sheria, kanuni na taratibu za forodha kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji, huku wakihakikisha wafanyabiashara wanapata huduma bora na kwa wakati ili kuimarisha mazingira ya biashara na kuongeza imani ya wadau.
Alieleza kuwa Kituo cha Forodha cha Horohoro kina nafasi muhimu katika kurahisisha biashara kati ya Tanzania na nchi jirani, hususan Kenya, hivyo kuendelea kuboresha utendaji wake kutasaidia kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Ziara ya Waziri wa Fedha wilayani Mkinga imelenga kutathmini utendaji wa taasisi za ukusanyaji wa mapato, kusikiliza changamoto zinazozikabili pamoja na kuhimiza uwajibikaji na usimamizi madhubuti wa rasilimali za Serikali ili kuendelea kuimarisha uchumi na maendeleo ya nchi.



Comments
Post a Comment