MBUNGE wa Jimbo la Tarime Mjini, Mhe. Esther Matiko, amekabidhi mifuko 120 ya saruji kwa shule za msingi zilizopo katika kata za Sabasaba na Nyamisangura, Halmashauri ya Mji wa Tarime mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za kuboresha miundombinu ya elimu na kuweka mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mhe. Matiko amesema ofisi yake imekuwa ikipokea maombi mengi kutoka kwa shule, taasisi mbalimbali pamoja na wananchi wanaohitaji msaada wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Alisema pamoja na mahitaji kuwa makubwa kuliko uwezo uliopo, ataendelea kushirikiana na Serikali, viongozi wa ngazi mbalimbali na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha changamoto zinazokabili sekta ya elimu zinapatiwa ufumbuzi.
"Tumekuwa tukipokea maombi mengi kutoka shule na taasisi mbalimbali. Mahitaji ni mengi sana, lakini kwa ushirikiano wetu na wadau wa maendeleo tutaendelea kuyashughulikia hatua kwa hatua ili kuboresha mazingira ya watoto wetu ya kujifunzia," amesema Matiko.
Mbunge huyo ameeleza kuwa elimu ni msingi wa maendeleo ya taifa, hivyo ni jukumu la kila mmoja kushiriki katika kuimarisha miundombinu ya shule ili wanafunzi wapate mazingira salama na rafiki ya kujifunzia.
Amebainisha kuwa msaada huo wa saruji utatumika katika ukarabati wa madarasa pamoja na miundombinu mingine muhimu inayohitaji maboresho katika shule hizo.
Aidha, amewataka wakuu wa shule, kamati za shule, madiwani na wananchi kuhakikisha vifaa hivyo vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kusimamiwa kwa uwazi na uadilifu ili viweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa kwa manufaa ya wanafunzi na jamii kwa ujumla.
Matiko pia amewapongeza viongozi wa kata, madiwani, kamati za ujenzi wa shule, walimu na wadau mbalimbali wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana katika kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya elimu ndani ya Jimbo la Tarime Mjini.
Amesema mafanikio yanayopatikana katika shule mbalimbali ni matokeo ya mshikamano na ushirikiano kati ya wananchi, viongozi na wadau.
"Maendeleo haya hayawezi kuletwa na mtu mmoja. Yanahitaji ushirikiano wa wananchi, viongozi na wadau wote wenye mapenzi mema na elimu. Nawaomba tuendelee kushikamana ili kuhakikisha watoto wetu wanapata mazingira bora ya kusoma," amesisitiza.
Pia amewapongeza viongozi pamoja na wadau wa maendeleo ikiwemo Nyansaho Foundation Kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo ikiwemo pia kampuni ya Soya one.
Ameongeza kuwa msaada huo ni sehemu ya mpango mpana wa kuendelea kuimarisha miundombinu ya elimu katika jimbo hilo, akiahidi kuendelea kutafuta rasilimali na kushirikiana na Serikali Kuu pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha shule nyingi zaidi zinanufaika na miradi ya maendeleo kwa lengo la kuinua kiwango cha elimu na kuandaa kizazi chenye uwezo wa kulijenga taifa.





Comments
Post a Comment