Na John Mapepele, Addis Abbaba
Waziri wa Afya, Mheshimiwa Mohamed Omari Mchengelwa, leo Februari 14, 2026 amekutana na Makamu wa Rais wa Susan Thompson Buffet Foundation (STBF), Prof Senait Fisseha, jijini Addis Ababa kwenye Mkutano wa pembezoni mwa kilele cha Kongamano la 39 la Umoja wa Afrika na kufanya mazungumzo ya kimkakati katika kukabiliana na changamoto ya vifo vya mama na mtoto.
STBF ni miongoni mwa wafadhili wakubwa wa Serikali katika uimarishaji wa mifumo ya afya hususani katika kupunguza vifo vitokanavyo uzazi.
Aidha, Mheshimiwa Waziri Mchengerwa akiwa na Katibu Mkuu, Dkt. Seif Shekalaghe amelishukuru STBF kwa msaada wa fedha wa kiasi cha Dola za Marekani milioni 36.8 zilizotolewa kati ya 2021 - 2025 ambazo zimesaidia katika kuimarisha mifumo ya afya na hivyo kuchangia katika kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi, watoto na vijana.
Mheshimiwa Mchengerwa alichukuwa fursa hii kumuomba Prof. Sinait kuangalia mpango wa Tanzania wenye nia kuendeza ajenda ya kukinga na kuzuia vifo vitokanavyo na uzazi kupitia uimarishaji wa mifumo ya afya.
Kwa upande wake, Prof. Fisseha ameshukuru kwa ushirikiano uliopo baina ya Taasisi yake na Serikali ya Tanzania katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi huo.
"Ninashukuru kuona kuwa ajenda ya kukinga na kuzuia vifo vitokanavyo na uzazi Afrika ipo mikononi mwa Rais mwanamke Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye amefanya kazi nzuri ". Amefafanua Prof. Fisseha
Vilevile ameahidi kuwa STBF litaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuweka raslimali fedha ili kuimarisha mifumo ya afya kwenye huduma za mama na mtoto.
Tanzania ni nchi inayopigiwa mfano na nchi za Umoja wa Afrika kwa kufanya vizuri katika kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.






