Watoto watatu kati ya sita kutoka nchini Burundi wenye matatizo ya matundu ya moyo wamefanyiwa upasuaji wa kuziba matundu hayo kwa mafanikio katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), hatua inayodhihirisha uwezo wa Tanzania katika huduma za kibingwa na kuimarisha ushirikiano wa afya katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Huduma hiyo imetolewa kupitia ushirikiano kati ya Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) na wataalamu wa afya kutoka Burundi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza tiba utalii na kubadilishana utaalamu wa kitabibu.
Akizungumza na waandishi wa habari Julai 9, 2026 jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Prof. Abel Makubi, alisema watoto wote waliopatiwa matibabu wanaendelea vizuri na wameonyesha maendeleo ya kuridhisha baada ya kufanyiwa upasuaji huo.
“Mafanikio haya yanaonyesha uwezo wa taasisi zetu za afya kushirikiana kutoa huduma za kibingwa zinazokidhi viwango vya kimataifa. Ushirikiano huu pia umefungua fursa ya kubadilishana ujuzi na uzoefu kati ya wataalamu wa Tanzania na Burundi,” amesema Prof. Makubi.
Amesema hatua hiyo inaendelea kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuwa kitovu cha huduma za afya za kibingwa katika ukanda huu, huku ikichochea maendeleo ya tiba utalii na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya afya.





Comments
Post a Comment