Na: Dawati la Habari Polisi Geita
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limemfikisha mahakamani Lufuta Magoma (40) Mganga wa Kienyeji na mkazi wa kijiji cha Rutunguru akituhumiwa kwa mauaji ya Dotto Magoma Nyara (70) ambaye ni mama yake mzazi.
Mshtakiwa huyo amepandishwa kizimbani leo Ijumaa Julai 10, 2026, katika Mahakama ya Wilaya ya Chato na kusomewa shtaka la Mauaji.
Akisoma shauri hilo la jinai namba 15471 la mwaka 2026 mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Chato, Mhe. Erick Kagimbo, Wakili wa Serikali Mashaka Said, aliieleza mahakama kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo mnamo tarehe 04.06.2026 katika Kijiji cha Rutunguru, wilaya ya Geita.
Mshtakiwa akiwa katika eneo la Rutunguru anadaiwa kumshambulia na kumuua Mama yake mzazi kinyume na kifungu cha 196 na 197 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2023.
Hata hivyo, mshtakiwa huyo hakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kisheria ya kusikiliza mashauri ya mauaji.
"Mahakama haina mamlaka ya kusikiliza shauri hili, kwa hiyo hautatakiwa kujibu chochote juu ya tuhuma zinazokukabili. Vilevile, kesi inayokukabili haina dhamana, hivyo utaendelea kuwa mahabusu hadi pale upelelezi utakapokamilika," alisema Hakimu Kagimbo.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 23, 2026, na mshtakiwa amerejeshwa rumande.


Comments
Post a Comment