JUMLA ya sh. trilioni 1.77 zinahitajika kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, maabara, ajira mpya za walimu, ruzuku ya mitihani, ya vitabu na uendeshaji kwa wanafunzi zaidi ya milioni tatu wanaotarajiwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2028.
Hayo yamesemwa Bungeni, jijini Dodoma leo (Jumatano, Aprili mosi, 2026) na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba wakati akiwasilisha Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027.
“Tathmini inaonesha kuwa wanafunzi 3,021,177 wanatarajiwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2028. Jumla ya gharama zinazohitajika ni shilingi trilioni 1.77 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 23,226; matundu ya vyoo 46,632; maabara 9,366; ajira mpya za walimu 40,192; ruzuku ya vitabu na uendeshaji pamoja na ruzuku ya mitihani na upimaji,” amesema.
Amesema mahitaji hayo yanatokana na uamuzi wa Serikali kuimarisha sekta ya elimu kwa kuzingatia Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 (Toleo la 2023), mitaala iliyoboreshwa, mipango na mikakati mbalimbali ikiwa na lengo la kuzalisha rasilimaliwatu wenye ujuzi na maarifa stahiki yatakayowezesha kumudu ushindani wa ajira na uwezo wa kujiajiri ndani na nje ya nchi.
Amewataka Wakuu wa Mikoa wasimamie kikamilifu maandalizi na mapokezi ya wanafunzi wa elimumsingi ya lazima ya miaka 10 watakaojiunga na kidato cha kwanza mwaka 2028 kwa kukamilisha miundombinu na huduma zote muhimu.
“Tunaposema elimu ya lazima kuwa miaka 10, kimsingi tunasema tulikuwa na sekondari kila kata, sasa tunaongelea kuwa na shule ya sekondari kila kijiji. Lazima tujiandae kwa miundombinu pamoja na maoteo ya mahitaji yote ya kutekeleza mpango huo.”
Amesema ili kuhakikisha wanafunzi wote wanapata nafasi ya kuendelea na masomo, katika mwaka wa fedha ujao, Serikali imetenga sh. bilioni 139.28 kupitia mapato ya ndani ya halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 4,193 na matundu ya vyoo 13,943. Na kupitia Serikali Kuu, Waziri Mkuu amesema, zimetengwa sh. bilioni saba kwa ajili ya ujenzi wa maabara 233.
Alielezea kuhusu ujenzi wa shule mpya za sekondari za amali, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imetoa sh. bilioni 88.84 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya 103 za amali. “Kati ya hizo, ujenzi wa shule 27 umekamilika na zinatumika. “Hadi kufikia Februari, 2026 shule 158 za sekondari ya chini (O’ level) zinatekeleza mkondo wa amali wa mitaala iliyoboreshwa ikilinganishwa na shule 41 zilizoanza mwaka 2024,” amesema.
“Ili kuboresha ufundishaji wa masomo ya amali, Serikali imepeleka walimu 150 kwenye mafunzo ya muda mfupi nchini India. Aidha, walimu 156,948 kati 172,609 kutoka shule za msingi 17,111 pia walishiriki mafunzo endelevu kazini.”
Akielezea utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2025/2026, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya ujenzi wa shule mpya za msingi 277. “Serikali imeongeza miundombinu katika shule za msingi na sekondari zilizopo kwa kujenga madarasa 5,439, majengo ya utawala saba, mabweni 21, hosteli 26, nyumba za walimu 69, maabara 46, mabwalo matano na vituo vya walimu 70.
Akifafanua kuhusu ukarabati wa shule, Waziri Mkuu amesema Serikali imekamilisha ukarabati wa shule za msingi 228 na ujenzi wa miundombinu iliyojengwa kwa nguvu za wananchi ikiwemo maboma 132 ya mabweni ya shule za sekondari, vyumba vya madarasa 697 katika shule za msingi na vyumba vya maabara 175 katika shule za sekondari.
Waziri Mkuu ametua fursa hizo kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka vifaa vya maabara katika shule za sekondari 231 zikiwemo shule mpya 26 maalumu za kitaifa za sayansi za wasichana.
Mbali na hilo, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kutekeleza Mpango wa Elimu Bila Ada kwa kugharimia elimu ya awali hadi elimu ya sekondari ya juu ambapo hadi kufikia Februari, 2026 shi. bilioni 383.22 kati ya sh. bilioni 510.96 sawa na asilimia 75 zilikuwa zimetolewa kwa shule za msingi 18,119 na shule za sekondari 5,179.
Kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe sh. trilioni 12.5 kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake ambapo kati ya fedha hizo, sh. trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe sh. bilioni 225 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge ambapo kati ya fedha hizo, sh. bilioni 207.99 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. bilioni 17.02 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.





