Na MASHAKA MHANDO, Tanga
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira imeeleza kuridhishwa na maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa maji wa Hatifungani ya Kijani (Green Bond) wenye thamani ya Shilingi Bilioni 53.3, unaolenga kumaliza kero ya upatikanaji wa huduma hiyo kwa wakazi wa Jiji la Tanga na wilaya jirani.
Akizungumza jana wakati wa ziara ya kukagua miradi inayotekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA), Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Jackson Kiswaga, amesema ujenzi huo umefikia asilimia 65 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba mwaka huu.
Mhe. Kiswaga amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu ushiriki wa sekta binafsi katika uzalishaji wa maji, huku akiitaka Wizara ya Maji kuhakikisha wakandarasi wanalipwa kwa wakati ili wasikwamishe kasi ya ujenzi.
"Tunamshukuru Rais kwa kutoa Shilingi Bilioni 35 kwa ajili ya mradi wa Mkinga-Horohoro kupitia fedha za ndani. Kamati inataka kuona mradi huu unakamilika kwa wakati ili ifikapo mwaka 2030, malengo ya Serikali ya kufikisha maji kwa asilimia 100 yawe yametimia," amesema Kiswaga.
Awali, Mkurugenzi wa Tanga UWASA, Mhandisi Godfrey Hills, alibainisha kuwa mradi huo unajumuisha upanuzi wa kituo cha kusukuma maji cha Mabayani kutoka lita milioni 42 hadi milioni 72 kwa siku, na ukarabati wa mtambo wa Mowe utakaofikisha uzalishaji wa lita milioni 60 kwa siku.
Naye Meneja wa RUWASA Mkoa wa Tanga, Mhandisi Upendo Lugongo, amesema hadi sasa mkoa unafikia asilimia 79 ya upatikanaji wa maji, huku wilaya ya Mkinga ikitarajiwa kupanda kutoka asilimia 72.1 hadi 89.03 mara baada ya mradi wa Mkinga-Horohoro kukamilika wenye thamani ya shilingi bilioni 35 utakapokamilika.
Kamati ya Bunge imekagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo ambao katika awamu yake ya kwanza unatarajiwa kuhudumia jumla ya vijiji 17 ndani ya wilaya hiyo.
Mhandisi Upendo alisema mradi huo kwa ujumla umefikia asilimia 65 ya utekelezaji wake. Katika ziara hiyo, Kamati imezindua rasmi upatikanaji wa maji katika Kata ya Mtimbwani, ambapo wananchi wa eneo hilo sasa wameanza kupata huduma ya maji safi ya bomba, ikiwa ni sehemu ya mafanikio ya awali ya mradi huo mkubwa utakaohudumia vijiji 37 utakapokamilika kikamilifu.
Katika ziara hiyo, Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso, amempongeza mkandarasi wa STC kwa kazi nzuri, huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia ubora wa huduma na kuwashirikisha watu binafsi katika usambazaji ili kuwafikia wananchi wa vijijini haraka zaidi.
Wajumbe wa Kamati, akiwemo Mbunge wa Bumbuli mhandisi Charles Singano na Makamu Mwenyekiti Pius Lyanda, wameshauri Serikali kutenga bajeti maalumu kwa ajili ya kuhifadhi vyanzo vya maji na bwawa la Mabayani ili kuzuia uharibifu wa mazingira unaotokana na shughuli za kibinadamu.
Kwa upande wao, wakazi wa kijiji cha Manza wakiongozwa na Rashid Ibrahim na Mariam Said wamemshukuru Rais Samia kwa mradi huo wakieleza kuwa ni ukombozi utakaowapunguzia adha ya kutafuta maji na kuwawezesha kujikita katika shughuli za kiuchumi.







