Jumla ya Wakazi 600 wa Kitongoji cha Makundusini, Kijiji cha Singu Kata ya Kukirango Wilaya ya Butiama mkoani Mara wamenufaika na Mradi wa Maji uliofanikishwa na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Butiama Mhe. Jumanne Abdallah Sagini kupitia Taasisi ya Direct Aid Society Tawi la Tanzania kutoka Kuwaït.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Kisima cha Maji chenye uwezo za kuzalisha zaidi ya lita 20000 kwa siku, Mgeni Rasmi katika hafla hiyo Mkuu wa Wilaya ya Butiama Mhe. Thecla Mkuchika amepongeza juhudi zilizofanywa na Mbunge Mstaafu wa Jimbo hilo Mhe. Jumanne Sagini kwa kitendo cha kuunga mkono Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sera ya kumtua ndoo mama kichwani pia amesema mradi huo utapelekea kuondokana na magonjwa yanayosababishwa na matumizi ya maji yasiyo safi na salama.
Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi wa Taasisi ya Direct Aid Society Tawi la Tanzania kutoka Kuwaït Bw. Abdelhamid Ismail amesema kuwa taasisi ilianza kutoa huduma nchini tangu mwaka 1987 na tayari wapo katika Kanda tano ambazo ni Tanga, Moshi, Kigoma, Singida na Dar es Salaam na hivyo kupatikana kwa mradi wa Kisima cha Maji Kitongoji cha makundusini ni urafiki na mahusiano mazuri kati yao na Mhe. Jumanne Abdallah Sagini ambapo aliwaunganisha na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania.
Nae Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Mara Msabaha Kassim amesema kuwa kuwepo kwa mradi huo ni mawazo ya Mhe. Jumanne Abdallah Sagini tangu aliponunua eneo hilo kulikabidhi BAKWATA walishirikiana vyema na akawa na mikakati ya kupeleka miradi mingi maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Butiama ikiwemo huu wa kisima cha maji.
Diwani wa Kata ya Kukirango Mhe. Rajab Mjengwa ameeleza kuwa ni jukumu lao kuhakikisha huduma inaendelea kupatikana kwa wakazi wote wa Kitongoji cha makundusini na vitongoji jirani. Pia Diwani wa Viti maalumu Wilaya ya Butiama Mhe. Amina Ally Solis ameshukuru kuwepo kwa mradi huo kwani umepunguza adha ya kina mama na watoto waliokuwa wanatembea zaidi ya kilometa sita kutafuta maji.
Aidha Mwenyekiti wa Kijiji cha Singu Bitarus Mkono kwa niaba ya wananchi wa kijiji hiko amewashukuru wafadhili wa Taasisi ya Direct Aid Society Tawi la Tanzania nchini Kuwaït na Mbunge aliyepita Mhe. Jumanne Sagini kwa kuwasilikiliza na kutatua kero mbalimbali za wananchi ikiwemo ya maji kijijini hapo.




