Mwigulu Nchemba: Kutoka kuchunga ng'ombe hadi Uwaziri Mkuu wa Tanzania

GEORGE MARATO TV
0




Mwigulu Lameck Nchemba Madelu ni Waziri Mkuu mpya wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni mwenyeji wa mkoa wa Singida na kwa sasa ana umri wa miaka 50.


Uteuzi wake umetangazwa rasmi bungeni mjini Dodoma, katikati mwa Tanzania  na baadaye kuthibitishwa na bunge, kwa mujibu wa Katiba ya nchi . Amethibitishwa kwa kura 369 za ndio kati ya 371 zilizopigwa na wabunge mbili zikiharibika.


Mwigulu anajulikana kama mfano wa mafanikio yanayotokana na bidii na kujituma. Alikulia katika mazingira ya kijijini na alitoka katika familia yenye hali ya kawaida, ambapo aliwahi kuchunga ng'ombe nyikani akiwa kijana mdogo. Maisha hayo yalimfundisha nidhamu, uvumilivu na kuthamini kazi halali. Mara kadhaa amekuwa akisimulia hadithi ya maisha yake kama njia ya kuwahamasisha vijana kupambana kupitia elimu na kujituma.


"Mimi umasikini wa Tanzania sijausoma kwenye kitabu nimeuishi, miaka takribani 32 nimeishi katika maisha hayo ya umasikini", alisema Nchemba mara baada ya kuthibitishwa bungeni. "Unaenda kuchunga ukirudi nyumba nzima inavuja, natambua maisha haya". Anasema Nchemba.


Alisoma shule ya msingi Makunda mkoani Singida kati ya mwaka 1987 hadi 1993, kisha akaendelea na masomo ya sekondari katika shule ya sekondari Ilboru mkoani Arusha na sekondari ya Mazengo mkoani Dodoma ngazi ya kidato cha tano na sita. Baada ya hapo alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambako alisomea shahada ya kwanza ya uchumi na baadaye akahitimu shahada ya uzamili mwaka 2006, na baadaye kupata shahada ya uzamivu kutoka chuo hicho hicho.


Safari ya kisiasa ya Mwigulu


Safari yake ya kisiasa ilianza kupanda kasi mwaka 2010 aliposhinda ubunge wa Jimbo la Iramba Magharibi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Alirudi tena bungeni mwaka 2015. Ndani ya chama chake amejipatia heshima kama kiongozi mwenye msimamo thabiti na anayejali nidhamu katika utumishi wa umma. Amewahi kuwa Katibu Mkuu Msaidizi, mjumbe wa Kamati Kuu, Halmashauri Kuu na sekretarieti ya chama kwa miaka mingi.


Dkt. Mwigulu amewahi kushika nafasi mbalimbali serikalini. Alianza kama Naibu Waziri wa Fedha katika serikali ya awamu ya nne chini ya Rais Jakaya Kikwete. Baadaye aliteuliwa kuwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi mwaka 2015, kabla ya kuhamishiwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi mwaka 2016. Mwaka 2021 aliteuliwa kuwa Waziri wa Fedha, nafasi aliyoishikilia hadi uteuzi wake kuwa Waziri Mkuu.


Mwaka 2018 aliondolewa katika nafasi ya Waziri wa Mambo ya Ndani baada ya Rais wa wakati huo, John Magufuli, kueleza kuwepo kwa changamoto katika wizara hiyo ikiwemo matumizi mabaya ya fedha na kasoro katika baadhi ya mikataba ya serikali. Pia alimlaumu kwa kutumia muda mwingi katika mitandao ya kijamii badala ya kufanya kazi za umma ikiwemo kudhibiti ajali za barabarani. Hata hivyo, Mwigulu aliendelea kuwa miongoni mwa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa ndani ya chama chake.



Hamia Burundi" kauli tata ya Mwigulu inayoishi


Kauli yake maarufu iliyoibua mjadala mkubwa ilitolewa mwaka 2021 alipokuwa akiwasilisha bajeti akiwa Waziri wa Fedha. Baada ya kuulizwa kuhusu malalamiko ya wananchi juu ya kodi kwenye miamala ya simu, alisisitiza kuwa sheria ikishapitishwa na bunge haina budi kutekelezwa, akiongeza kwa utani kwamba "anayehisi afadhali kuhamia Burundi, basi aende tu." Kauli hiyo ilitawala mijadala kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari kwa muda mrefu.


Mwigulu ni mtu anayejulikana kwa uzalendo wake. Mara nyingi huonekana akiwa amevalia skafu yenye rangi za bendera ya taifa, akisisitiza umuhimu wa kuipenda Tanzania. Pia amekuwa akisaidia vijana hasa katika masuala ya elimu, akiamini kuwa elimu ndiyo njia kuu ya kupambana na umasikini.


Uteuzi wake kuwa Waziri Mkuu uliwashangaza watu wengi, kwani jina lake halikuelezwa sana katika mijadala ya awali. Wakati wa uteuzi huo, majina kama ya Dk. Tulia Ackson, Paul Makonda, Profesa Kitila Mkumbo na Dotto Biteko ndiyo yalikuwa yakitajwa zaidi. Hata hivyo, Rais alimteua Mwigulu kutokana na uzoefu wake serikalini na uwezo wake wa kuongoza shughuli za serikali bungeni kwa ufanisi.


Uteuzi wake umeleta hisia mseto



Mmoja wa wabunge wa muda mrefu, William Lukuvi alisifu uteuzi wake.


"Tunajua uvumilivu alionao Mwigulu kwa mema na mishale mingi aliyopigwa lakini hajatetereka" alisema Lukuvi. Huku Mwanasheria Mkuu, akiongeza "Kwa uzoefu wa Mwigulu Nchemba ni mtu sahihi wa nafasi hii ya uwaziri mkuu".


Hata hivyo, wapo wanaona, Nchemba ni sura ilele ile kwenye serikali ile ile, ingawa uteuzi wake haukutarajiwa.


"Uteuzi wake haukutarajiwa na wengi, majina yaliyokuwa yanatajwatajwa halikuwepo kabisa, ila sidhani kama analeta kitu kipya sana, kwa kuwa amekuwa serikali kwa zaidi ya muongo mmoja na kwa nafasi nyeti", alisema mmoja wa wanahabari wa siasa za Tanzania.


Mbunge wa upinzani kutoka ACT- Wazalendo Addo Shaibu mbali na kuunga mkono uteuzi wake. "Ni mtu mchapakazi, kwetu sisi tulio wachache tunakuunga mkono, kama ishara ya kukupesha imani, tukiwa na imani kwamba utachapa kazi. Tunaimani utasimamia vizuri serikali na rasilimali za taifa, na utasimamia maboresho ya upatikanaji wa katiba mpya", alisema Addo.


Baada ya kuthibitishwa na Bunge, Nchemba alisema "Natambua ukubwa wa kazi iliyo mbele yetu, kazi kubwa kwa watanzania wote", alirejea Dira ya Tanzania ya 2050, akisema imewalenga vijana aiongezea kusimamia upatikanaji wa ajira karibu milioni 8.


"Watanzania wote watasikilizwa katika ofisi za umma", ilikuwa kauli iliyoshangiliwa bungeni, akionyesha anakuja kuleta jambo jipya kwenye utendaji wa Serikali. Aliwatahadharisha watumishi wa Serikali, "Nitakuja na fyekeo na rato".


"Bila amani haya yote hayawezi kufikiwa, tumtangulize Mungu" alimaliza hotuba yake ya kwanza bungeni baada ya kuthibitisha Novemba 13, 2025.


Nchemba anakuwa Waziri Mkuu wa 12 wa Tanzania, akifuata nyayo za Mawaziri wengine Wakuu Tanzania, Julius Kambarage Nyerere 1960-1962, Rashidi Kawawa 1962–1962 na tena 1972–1977, Edward Moringe Sokoine 1977-1980 na 1983-1984 na Cleopa David Msuya 1980–1983 na tena 1994-1995.


Wengine ni Salim Ahmed Salim 1984–1985, Joseph Sinde Warioba 1985–1990, John Malecela 1990-1994, Frederick Sumaye 1995-2005, Edward Lowassa 2005-2008, Mizengo Pinda 2008–2015 na Kassim Majaliwa 2015-2025, anayemaliza muda wake sasa.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top