Na Shomari Binda-Musoma
MKUU wa mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi amezindua rasmi shule ya sekondari Muhoji iliyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi.
Shule hiyo ameizindua jana juni 9,2025 Kijijini Muhoji Kata ya Bugwema huku akiwapongeza wananchi na mbunge wa jimbo la Musoma Vijijini Profesa Sospeter Muhongo kwa kuanza ujenzi kwa kutumia nguvu na kuchangia fedha zao.
Hii ni sekondari ya pili ya Kata hiyo yenye vijiji vinne vya Bugwema, Kinyang'erere, Masinono na Muhoji.
Akizungumza kwenye uzinduzi huo mkuu huyo wa mkoa ambaye alikuwa mgeni rasmi amewaeleza wananchi wa Kata ya Bugwema dhamira nzuri na yenye manufaa makubwa ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ya uwekezaji mkubwa anaoufanya kwenye sekta ya elimu.
Amesema kuendelea kuwekeza huko ni kuhakikisha shule zinajengwa karibu na wananchi kuhakikisha wanafunzi hawatembei umbali mrefu kwenda shuleni.
Kanali Mtambi amesema hakuna urithi ulio bora kama elimu na kutoa wito kwa wanafunzi kusoma kwa bidii na wazazi na walezi kusimamia elimu ya watoto.
" Serikali ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan imeleta fedha hapa zaidi ya milioni 175 kwaajili ya ujenzi wa shule hii ili kufanya uwekezaji kwenye sekta ya elimu.
" Lakini nitumie nafasi hii kuwapongeza wananchi na mbunge wenu Profesa Sospeter Muhongo kwa kuanza ujenzi wa shule hii kwa kutumia nguvu zenu na michango yenu"amesema.
Ujenzi wa shule hiyo ulianza disemba 2022 kwa kutumia michango ya fedha iliyopatikana kwenye harambee iliyoongozwa na Mbunge wa Jimbo hilo Prof.Sospeter Muhongo
Gharama za ujenzi huo hadi sasa umefikia shilingi milioni 175,346,955 huku wachangiaji wakuu wakiwa serikalj kuu milioni 75,mfuko wa jimbo milioni 24.4,Wanakijiji fedha na nguvu kazi,Halmashauri (Musoma DC),Wazaliwa wa Kijiji cha Muhoji,Wadau wa Maendeleo na Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Profesa Sospeter Muhongo.
Miundombinu iliyopo ni vyumba vya madarasa vinne (4), ofisi moja (1) ya walimu, matundu 17 ya vyoo vya wanafunzi na walimu
Miundombinu ya elimu iliyopangwa kuendelea kujengwa ni vyumba vya madarasa, maabara za masomo ya sayansi, maktaba, chumba cha TEHAMA, Jengo la utawala na nyumba za kuishi walimu
Shule tayari imefungiwa umeme na iko kwenye mradi wa kufungiwa maji ya bomba huku wananchi wakimuomba mkuu wa mkoa kumfikishia salamu Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan na kuahidi kumchagua kwa kura nyingi kwenye uchaguzi wa mwezi oktoba mwa huu.
Wakati huo huo mbunge wa jimbo hilo Profesa Sospeter Muhongo amegawa vitabu 2 namba 6 na 6 vya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2020-2025 kwa wananchi na viongozi walioshiriki sherehe hizo.