📌 Zabuni ya ujenzi wa kituo hicho kutangazwa Jumatatu
Na Mwandishi Wetu, Muheza
NAIBU Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Hamisi Mwinjuma maarufu MwanaFA, amesema kukosekana kwa kituo cha afya tarafa ya Amani kulikuwa kukimkosesha usingizi kwa kuwa hakutaka miaka yake mitano ya awali ya ubunge asimalize bila kupatikana kituo hicho.
Akizungumza katika hafla fupi ya kukabidhi kiasi cha shilingi milioni 645.2 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo hicho iliyofanyika katika eneo litakalojengwa kwenye zahanati ya Kijiji cha Mgambo Miembeni, alisema suala la kituo lilitolewa ahadi na wabunge waliopita tangu mwaka 1998.
Alisema kituo hicho kilikuwa na siasa kubwa kutoka kwa watangulizi wake wa nafasi hiyo, hivyo kupatikana kwa kituo hicho ni faraja kwake na Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya wabunge waliopita kutoa ahadi bila mafanikio.
"Nimewahi kuja Amani mara nyingi sana lakini leo, nimekuja kama kidume kweli kweli, mara hii nimekuja Kifua mbele kama nimepigwa ngumi ya mgongo," alisema na kuongeza,
"Nalisema hili kwasababu sisi wengine tuna sifa nyingi lakini sifa ya uongo sina, miongoni mwa mambo yaliyokuwa yakinilaza macho, yaliyokuwa yakinikosesha raha na miongoni mwa mambo yaliyokuwa yakitumika vibaya kisiasa ni hili la kituo cha afya tarafa ya Amani,".
Alisema anamshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kusikiliza maombi ya muda mrefu ya ujenzi wa kituo hicho yaliyowekwa na wabunge waliopita, hatimaye yeye amekwenda kutimiza ndoto za wananchi wa tarafa hiyo baada ya serikali kutoa fedha za ujenzi wake.
Alisema hoja ya kupata kituo cha afya tarafa ya Amani ilikuwepo tangu mwaka 1998 iliyoahidiwa na Julius Semwaiko aliyekuwa mbunge katika kipindi hicho na walipita wabunge wawili walishindwa na Sasa baada ya miaka 27, amefanikisha hilo.
Alisema mwaka 2023 aliwaeleza wananchi wa tarafa hiyo kwamba hadi ifikapo Juni mwaka huu endapo serikali isingetoa fedha hizo, angeanza ujenzi huo kwa kutoa shilingi milioni 100 ili wananchi waanze tofauti na aliyetoa matofari 500 kutaka kujengwa kituo hicho jambo ambalo alisema halikuwa sahihi na utani wa kisiasa.
"Subira mliokuwa nayo muda mrefu imezaa heri baada ya serikali kutoa fedha za mkupuo mmoja sh. 645,282,284 tofauti na maeneo mengine ambayo serikali inatoa fedha za kuanzia shilingi milioni 250," alisema MwanaFA.
Alisema dhamira yake ilikuwa ya dhati kabisa kuhakikisha kituo hicho kinajengwa kumaliza ndoto ya wananchi katika miaka yake ya kwanza ya ubunge katika Jimbo hilo ili wananchi waondokane na tatizo la kufuata huduma za Afya mbali na tarafa hiyo.
Mbunge huyo alidokeza kwamba serikali pia imetoa shilingi milioni 250 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo kingine cha afya katika tarafa ya Ngomeni ambacho kitajengwa kata ya Misozwe ili kukamilisha tarafa zote nne za wilaya hiyo kupata vituo vya afya.
Tarafa nyingine ni ya Bwembera iliyokuwa na kituo cha afya kilichojengwa kata ya Kwafungo, tarafa ya Muheza iliyokuwa na vituo vya afya viwili kata ya Mkuzi na Mbaramo.
Akizungumzia kuhusu barabara MwanaFA ambaye wananchi wilayani hapa wanampenda kutokana na kuleta miradi mingi, alisema kuwa awali barabara ya Muheza-Amani yenye urefu wa kilomita 32 ilikuwa imewekwa lami kilomita 4 tu.
Lakini Sasa kwa miaka minne hii tayari MwanaFA amefanikisha barabara hiyo kufikia kilomita 13 kwa kiwango cha lami.
"Ndugu zangu mlinisikia Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alipokuja Muheza nikimuomba kuhusu barabara hii na serikali katika mwaka huu wa fedha imenipa tena fedha za kujenga kilomita 4," alisema na kuongeza,
"Najua barabara hii bado inachangamoto kwa baadhi ya sehemu lakini mnaona wakandarasi wapo kazini wanajenga sehemu korofi kwa kuweka zege ili ipitie lakini niwaahidi nitaimaliza,".
Aliwataka wananchi wa tarafa hiyo kushirikiana na mafundi watakaojenga kituo hicho cha afya na wawe walinzi wa vifaa kuzuia watu wasiibe ili jengo hilo likamilike kwa wakati na kwa thamani ya fedha zilizotolewa.
Awali mganga Mkuu wa wilaya ya Muheza Dkt Fani Mussa alisema kituo hicho ambacho zabuni yake itatangazwa Juni 16 mwaka huu, kitahudumia wakazi 39,792 kutoka kata sita za Kisiwani, Amani, Mbomole, Kwezitu, Zirai na Misalai.
Dkt Fani alimshukuru mbunge huyo katika kipindi chake kufanikisha idara ya afya kupokea kiasi cha sh. 6,542,584,369.6 ambazo zimetumika kwa kujenga miundombinu, ununuzi wa magari, madawa na vifaa tiba.
Katibu wa CCM wilaya ya Muheza Simon Leng'ese alisema kuwa chama hicho kimefurahishwa na kazi nzuri iliyofanywa na serikali kutoa fedha hizo ambazo zimeweza kutekeleza ilani ya Chama hicho kwa vitendo na kwamba kituo hicho kitaipa heshima serikali pamoja na chama kwa kuwa kimesubiriwa kwa muda mrefu.
"Huu mradi ulishindikana muda mrefu Sasa MwanaFA ameweza, Mama Samia hoyeee, mbunge hoyeee," alisema Leng'ese ambaye aliwataka wananchi wawaunge mkono viongozi wanaotatua changamoto zao.
Katibu wa Uenezi na siasa wa wilaya ya Muheza Mwedi Sufiani alisema wakati umefika kwa wananchi wa Muheza kuchagua watu wenye maarifa ya kutatua changamoto zao kamwe wasichague watu wanaowapa fedha wakati wa chaguzi.
"Tunataka viongozi wenye akili wanaoleta maendeleo kwa watu wake, siyo mtu anayetumia fedha lakini akashindwa kuleta maendeleo," alisema Mwedi.
Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wilayani Muheza (UVCCM) Aziza Mshakangoto alimshukuru mbunge huyo kwa kufanikisha kituo cha afya na akawataka watu wanaotumia kituo cha afya kama mtaji wao kisiasa watafute kiki nyingine.
Aliwataka wananchi wa tarafa ya Amani wasiyumbe katika kuchagua wagombea ubunge na udiwani watazame watu walioleta maendeleo kikiwemo kituo hicho na waachane na watu wanaopitapita na kutoa sukari kwa watu wachache.
Diwani wa kata ya Misalai Said Mtunguja alimsifu mbunge kwa kusema kwamba katika kipindi chake amerahisisha kazi ya Siasa kwa kuwezesha wilaya hiyo kupata miradi mingi ya maendeleo katika kata zote za tarafa hiyo.
Alisema kuwa awali walianza ujenzi wa kituo hicho mwaka 2017 kwa kutumia michango ya wananchi lakini baada ya kuingia mbunge huyo alifuta michango hiyo na wananchi waliofunguliwa kesi kwa kutotoa michango kesi zao zilifutwa.
Hivyo, diwani huyo aliyesoma mistari mbalimbali ya biblia alisema kuwa Wagaratia sura 6 mstari 4 inasema "Kila mtu apimwe kwa kazi yake na ndipo azungumzie kazi ya mwenzake,".
Pia alinukuu kifungu cha biblia kutoa Mwanzo sura 43 mstari wa 45 kuwa "Chagueni mtu mwenye akili aweze kusimamia njaa ya watu kwa miaka Saba", alisema na kuongeza MwanaFA anaweza kusimamia njaa ya miaka Saba mara mbili.
Wananchi Mariamu Mtunguja na Said Baghaa waliahidi kumuunga mkono MwanaFA kutokana na kazi nzuri ambazo amezifanya katika tarafa hiyo ikiwemo kumaliza ndoto yao ya muda mrefu ya kupata kituo hicho cha afya.