Na MASHAKA MHANDO, Tanga
JESHI la polisi mkoani Tanga, limekutana na kuzungumza na madereva wa magari ya serikali, taasisi na mashirika ya umma kuwakumbusha umuhimu wa kuzingatia Sheria za usalama barabarani.
Akifungua mkutano baina ya jeshi hilo na madereva hao, Kamanda wa polisi mkoani Tanga ACP Almachius Mchunguzi, alisema kuwa kuna umuhimu mkubwa kwa madereva hao kuendesha magari hayo kwa kufuatia Sheria ili wasiweze kusababisha ajali za kizembe zinazotokana na mwendokasi.
Alisema wanawakumbusha Sheria hizo kwakuwa mara nyingi wao ndiyo wanaovunja Sheria hizo kwa kujiona wao hawapaswi kufuata Sheria kwa vile wamewapakia viongozi.
"Wakati mwingine mnawasingizia viongozi kwamba wao ndiyo wanawalazimisha mtembee mwendo mkali hapa, nyie ndiyo mliokuwa na dhamana ya kulitoa gari sehemu moja kwenda sehemu nyingine hivyo lazima mfuate Sheria za usalama barabarani," alisema Mchunguzi.
Akizungumza kuwaasa zaidi madereva hao, Mkuu wa usalama barabarani mkoani Tanga, SP Willy Mwamasika alisema kuwa madereva wengi wa magari ya serikali wanaona wao kama hawahusiki na sheria za usalama barabarani wakati sivyo.
Alisema baada ya mkutano huo dereva wa serikali atakayevunja Sheria za usalama barabarani watawachukulia hatua za kisheria.
Alisema hivi karibuni kumekuwa na wimbi kubwa la madereva wa magari ya serikali wanasababisha ajali ya kuwa viongozi wanaowaendesha na wengine kuwasababishia ulemavu.
"Tumeona tuwakumbushe, kwa wale ambao hawatafuata Sheria tutawachukulia hatua, dereva wa serikali kama dereva mwingine yeyote anapaswa afuate Sheria, umuhimu wa idara yako hakukufanyi uvunje Sheria," alisema na kuongeza "yapo magari ya jeshi, uokoaji na magari ya wagonjwa Wana Sheria zinazowaongoza lakini nao lazima wasingatie uendeshaji wa usalama barabarani,".
Akitoa mafunzo kwa madereva hao Mkuu wa usalama barabarani wilaya ya Tanga ASP Eliud Mwaisanila alisema dereva wa gari la serikali anapaswa azingatie Sheria ya usalama barabarani kifungu cha 2 sura namba 168 aliyofanyiwa marekebisho mwaka 2022.
Alisema dereva wa gari la serikali unapopata ajali licha ya kusababisha maafa na ulemavu lakini pia unaitia hasara serikali kwa kuharibu gari hilo.
"Unapopewa dhamana ya kuendesha gari la serikali lazima ulitunze na kuzingatia usalama wa watu unaowabeba, usiendeshe kwa shinikizo kwa kuvunja sheria za usalama barabarani.
Naye sajenti wa jeshi hilo SGT Cleopa Kitambi amewataka madereva hao wawe watulivu na wanaojiamini wakati wote wanapoendesha magari hayo kwa kutambua umuhimu wa usalama barabarani pindi wanapoona hatari mbele yao.
Mmoja waadereva hao wa serikali kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa wa Tanga, Leyla Mnaki alisema wamepokea mafunzo hayo na watazingatia Sheria hizo ili kuepusha ajali.
Leyla alikiri kwamba upo udhaifu kwa madereva hao pale wawapo kwenye misafara ya viongozi pale wanapoacha umbali mrefu kutumia mwendo kasi ili kuuwahi msafara huo jambo ambalo aliwaasa wenzake waache kufanya hivyo ili kuepusha kutokea ajali.
Kamanda wa polisi mkoani Tanga ACP Mchunguzi alisema mikutano na madereva wa serikali ambayo ni maagizo ya Mkuu wa jeshi hilo, yatafanyika wilaya zote za mkoa wa Tanga.

.jpg)










Comments
Post a Comment