WINDHOEK, Machi 22
Rais wa Namibia Netumbo Nandi-Ndaitwah, ambaye alichukua madaraka siku ya Jana Ijumaa, ametangaza timu yake mpya ya uongozi, ikiwa ni pamoja na uteuzi wa Lucia Witbooi kama Makamu wa rais na Elijah Ngurare kama waziri mkuu.
Akitangaza uteuzi huo siku ya Jumamosi huko Windhoek, mji mkuu wa nchi hiyo, Nandi-Ndaitwah, Rais wa tano wa Namibia, pia alianzisha marekebisho makubwa ya wizara na mashirika ya serikali ili kuimarisha ufanisi na kurahisisha shughuli."
"Kama viongozi waliochaguliwa, tuna jukumu kubwa la kuhakikisha kwamba tunaimarisha demokrasia, amani, utulivu na utawala bora nchini, na pia kuharakisha utoaji wa huduma bora za umma kwa Wanamibia wote," Nandi-Ndaitwah alisema katika taarifa yake.
Pia alitangaza kupunguza wizara za serikali kutoka 21 hadi 14, na Jumla ya manaibu waziri saba.
Akiangazia mabadiliko muhimu ya kimuundo, Nandi-Ndaitwah alisema kuwa mamlaka ya biashara sasa yatakuwa chini ya Wizara ya Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano ili kukuza diplomasia ya uchumi na kukuza ushirikiano wa kiuchumi wa kikanda na bara.
Ukuaji wa viwanda utahamia Wizara ya Madini na Nishati, ikiendana na jukumu lake katika kusimamia rasilimali za madini ili kuendesha ukuaji wa viwanda na mseto wa kiuchumi kupitia mipango ya uongezaji thamani, alisema.
Kuhusu sekta inayoibukia ya mafuta na gesi, alisisitiza kuwa usimamizi wake lazima uhakikishe manufaa ya juu kwa wananchi wote wa Namibia. "Kwa hiyo, usimamizi wa viwanda hivi utakuwa chini ya Ofisi ya Rais," aliongeza.



Comments
Post a Comment