Na Mwandishi Wetu, Muheza
NAIBU Waziri wa Habari Sanaa Utamaduni na Michezo, Hamis Mwinjuma maarufu MwanaFA leo tarehe 19 2025, amekabidhi bati 120 kwa ajili ya kuezekea nyumba ya mtendaji wa Umoja wa vijana (UVCCM) wilayani Muheza.
Akikabidhi bati hizo kwa Mwenyekiti wa UVCCM wilaya Muheza Aziza Mshakangoto, MwanaFA alisema ametekeleza ahadi yake ya kuziezeka nyumba tatu za jumuiya za chama wilayani hapa kuunga mkono wazo la Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Ustadh Rajab Abdarahman Abdallah za kila wilaya mkoani hapa kujenga nyumba za watumishi wa Chama.
MwanaFA alisema kuwa katika kipindi cha miaka minne na nusu aliyokaa katika ubunge wilaya ya Muheza imepiga hatua ya maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo katika chama.
Alisema mwaka 1993 waliokuwa viongozi wa CCM katika wilaya hiyo, walitenga eneo la Kirumba lililopo kata ya Genge kujengwa nyumba za watumishi wa chama pamoja na ofisi za chama.
"Lakini Sasa ni miaka 32 watu walikuwa wanasema watajenga lakini hapakujengwa, tulipokuja sisi wathubutu ndiyo tumefanya haya, tumejenga.
Alisema wakati wanatoa wazo la kuihamisha ofisi ya Chama kutoka eneo la sokoni watu wana-CCM walipinga lakini sasa baada ya kuona wameanza ujenzi na unakwenda kwa kasi jengo la ofisi ya wilaya wanaunga mkono ujenzi huo.
Alisema jengo hilo litakuwa la kisasa na ubora mkubwa kuliko yote yaliyopo katika wilaya za mkoa wa Tanga.
MwanaFA alisifu ujenzi wa nyumba ya mtendaji wa UVCCM katika wilaya hiyo kuwa limejengwa kwa kudhingatia ubora na viwango vikubwa na yeye akiwa mjumbe wa zamani wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya hesabu za serikali za mitaa (LAAC), ameridhishwa na ujenzi huo.
Alimsifu mwenyekiti wa UVCCM wilaya hiyo Aziza Mshakangoto kuwa ni Mwenyekiti mwenye ubora wa usimamizi lakini pia amekuwa akifanya vema katika kuongoza jumuiya hatamu bora za kisiasa.
Akizungumza kuhusu maendeleo MwanaFA alisema kuwa wilaya hiyo katika miaka minne imepiga hatua na kazi ameifanya tofauti na watangulizi wake kwa kuwa na miradi mingi ya maendeleo, usimamizi wake, uhai wa chama na miradi yake ikiwemo kuitangaza wilaya hiyo.
"Muheza ya mwaka 2020 na ya sasa ni tofauti na hata suala la maji hivi sasa ni tofauti na zamani kwakuwa sasa yanapatikana na ukikamilika mradi wa Maji wa miji 28 hali itakuwa tofauti kabisa," alisema.
Awali akimkaribisha mbunge huyo kuzungumza mwenyekiti wa UVCCM wa wilaya hiyo Aziza Mshakangoto alisema kuwa wanamshukuru mbunge kwa kujitoa katika shughuli zao za maendeleo na wao hawatamuacha.
"Mheshimiwa mbunge kwa namna unavyojitoa kwa shughuli za vijana kutuunga mkono, hatutakuacha katika dhamira yako ya kugombea tena katika uchaguzi unaokuja," alisema mwenyekiti huyo.
Alimshukuru mbunge kwa shukrani alizompa kuhusu ujenzi wa nyumba hiyo akasema kuwa wameisimamia katika ubora ili jumuiya nyingine mkoani hapa wafike wajifunze kupitia ujenzi wa nyumba yao hiyo.
Katibu wa CCM wilaya ya Muheza Simon Leng'ese alimshukuru mbunge huyo kwa kujitoa na hata kufanikisha ndoto ya ujenzi wa jengo la utawala ya Chama pamoja na kuezeka nyumba za watumishi wa chama.







.jpg)




Comments
Post a Comment