Na Mashaka Mhando, Tanga
FAMILIA ya marehemu Amri Athumani Majuto 'King Majuto', imetoa msaada wa futari kwa watoto yatima wa kituo cha Goodwill Children Home kilichopo kata ya Tangasisi Jijini Tanga.
Akizungumza mara baada ya kukabidhi futari hiyo Leo Machi 18 2025, mmoja ya mke wa marehemu King Majuto, Aisha Mbwana Yusuph alisema wamekabidhi sadaka ya chakula kwa ajili ya watoto yatima hao.
Alisema wamesukumwa kutoa chakula hicho kutokana na uwepo wa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani lakini pia fedha walizopewa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kiasi cha shilingi milioni 30.
"Tupo kwenye mfungo wa Ramadhani mara nyingi heri nyingi zinapatikana katika kipindi hiki, hivyo tumeshirikiana na familia kutoa sadaka hii," alisema Aisha.
Mtoto mkubwa wa marehemu King Majuto, Othman Amri alisema kuwa lengo lao la kutoa futari hiyo ni kumshukuru pia Rais baada ya kuwapatia fedha hizo ambazo, wameweza nao kutoa sadaka hiyo ili kumuombea mzazi wao huyo.
Alisema fedha hizo wametoa futari hiyo pia kumuenzi marehemu Mzee wao ambaye alifariki Agosti 8 mwaka 2018 na kwamba msaada huo ni sehemu ya kumuombea licha ya kumsomea Dua mara kwa mara.
"Lengo Kuu kuja hapa ni kutoa shukrani zetu za dhati kwa mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, mama yetu mlezi tunamshukuru sana ametukabidhi fedha tasilimu shilingi milioni 30, lakini sisi tukasema tulifanye suala hili kumuenzi Mzee wetu kwa kutoa sadaka katika kituo cha watoto yatima," alisema Othman ambaye ni mpiga bass na mwimbaji wa bendi ya Tanga Beach Resort ya Jijini Tanga.
Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, ilimtunuku tunzo Mzee Majuto kwa kuwa muigizaji na mchekeshaji bora nchini fedha ambazo walikabidhiwa familia mwezi February mwaka huu.
Othman alitumia muda huo kuishukuru serikali kwa kumuenzi Mzee wao kwa kumpa tunzo kutokana na mchango wake wa usanii alioutoa wakati wa uhai wake.
Mtoto mwingine wa marehemu King Majuto, Mohammed Amri alisema kuwa Mzee Majuto wakati wa uhai wake alikuwa akitoa sadaka mbalimbali kwa makundi mbalimbali hapa nchini hivyo sadaka hiyo ni sehemu ya kumuenzi marehemu baba yako.
Alisema familia yao inasikia faraja kubwa kutokana na kutoa sadaka hiyo wakati wa Ramadhani ambapo pia walifanya hivyo mwishoni mwa mwaka jana katika eneo la Kiruku alipozikwa marehemu huyo.
Mkurugenzi wa kituo hicho cha watoto yatima cha Goodwill Children Home, Idarus Mussa Mohamed alishukuru msaada huo na kuuelezea kwamba utasaidia watoto hao wanaoishi katika kituo hicho.
Alisema kuwa kituo hicho kinachosaidia watoto yatima, walemavu na wazee, kilianzishwa mwaka, alishukuru familia ya King Majuto kwa kukichagua kituo chao na kutoa msaada wa futari.










Comments
Post a Comment