Kongamano la dharura la pamoja baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), la kujadili hali ya usalama Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo limeratibiwa kufanyika Jumamosi wiki hii Jijini Dar es Salaam, Nchini Tanzania.
Hii inafuatia makubaliano kati ya mwenyekiti wa SADC ambaye pia ni Rais wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa na mwenyekiti wa EAC, Rais William Ruto wa Kenya.
Kulingana na taarifa hiyo, Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania, amekubali kuandaa kongamano hilo huku Marais Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC) na Paul Kagame wa Rwanda, wakithibitisha Ushiriki wao.
Vile vile, Rais Ruto amethibitisha kuwa amejadiliana na Marais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini, Yoweri Museveni wa Uganda, na Hassan Sheikh Mohamud wa Somalia, huku wote wakitoa Uthibitisho wa Kuhudhuria kongamano hilo la dharura.
Chanzo;KBC