Na MASHAKA MHANDO, Mkinga
Na Hadija Bagasha Tanga,
Rais wa Jamuhuri ya muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan amesema Serikali inakwenda kutunga sera na sheria ili kuharakisha mkakati wa matumizi ya nishati safi na kuweza kufikia lengo la watumiaji asilimia 80 ifikapo 2030.
Rais Dkt Samia ameyasema hayo wakati wa uzinduzi wa usambazaji wa nishati safi ya kupikia na ugawaji wa mitungi ya gesi kwa wananchi Wilayani Muheza Mkoani Tanga.
Rais alisema kuwa sera hizo rafiki ambazo wanakwenda kuzitunza zitawezesha ushiriki wa sekta binfsi na makampuni yanayojihusisha na uzalishaji wa nishati safi ya kupikia kwa bei nafuu.
Alisema dhamira ya sasa kama tukiendelea kutumia kuni na mkaa kama nishati kuu ya kupikia tunakwenda kuwa na majanga ambayo yatasababisha kukauka kwa vyanzo vya maji kutokana na ukataji wa miti lakini pia upo uwezekano mkubwa wa kupata maradhi ya kifua kutokana na matumizi ya kuni.
"Kwasasa tulisema asilimia 80 ya watu wetu ikifika 2030 wawe na nishati safi ya kupikia na kwasasa tuko chini ya asilimia hiyo lakini kwa kasi tunayoendelea nayo nina hakika kabla ya kufikia 2030 tutakuwa tumefikia lengo tulilojiwekea kwenye mkakati wetu, "alisisitiza Rais Dkt Samia.
"Kukiwa na majanga kama vile ukame upatikanaji wa vyakula unakuwa shida na kusababisha ukosefu wa chakula pamoja na ukosefu wa maji kutokana na kuharibu miti iliyopo karibu na vyanzo vya maji hivyo lengo la kampeni hii ni kuhifadhi misitu ili kuweza kupata maji na kupunguza athari za mabadiliko ya tabia Nchi, "alisema Rais Dkt Samia.
Aidha Rais Dkt Samia aliiagiza Wizara hiyo kuendelea kusimamia vizuri huku akiwataka REA kuendelea na mkakati huo ambapo amesema Serikali itaendelea kutunga sera na sheria zitakazowafanya waendelee haraka na mkakati huo.
Katika hatua nyingine Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alisema awali wakati akimteua mbunge wa Muheza Hamis Mwinjuma maarufu MwanaFA kuwa Naibu Waziri pamoja na Nikki wa pili kuwa Mkuu wa wilaya, watu hawakumwelewa lakini vijana hao wanafanya vizuri katika nafasi.
MwanaFA ni Naibu Waziri wa Habari Sanaa Utamaduni na Michezo ambaye Rais amemwelezea kuwa amekuwa akifanya vizuri kuongea na vijana wenzie wasanii.
Akitoa taarifa fupi mbele ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga, amesema kuwa serikali imetoa mitungi ya gesi (LPG) 400,445 kwa ajili ya kusambazwa katika wilaya zote nchini, ambapo kila wilaya inapokea wastani wa mitungi 3,255.
Kwa wilaya ya Muheza, Naibu Waziri Kapinga amesema kuwa, mitungi hiyo imesambazwa na wananchi wameinunua kwa wingi kutokana na bei yake nafuu ya Shilingi 16,000 kwa mtungi mmoja, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kupunguza gharama za matumizi ya mwanzo kwa wananchi.
Katika awamu ya kwanza ya mpango huo, jumla ya mitungi 99,000 inasambazwa kote Tanzania Bara na Zanzibar.
Naibu Waziri huyo wa Nishati ameongeza kwa kusema kuwa, serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo inahakikisha upatikanaji wa majiko kwa bei ya ruzuku ili kuwawezesha wananchi kutumia nishati mbadala kwa gharama nafuu.
Hatua hii ni sehemu ya juhudi za serikali katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi na kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, kwa lengo la kulinda mazingira na kuboresha maisha ya wananchi.
Naibu Waziri wa Habari, utamaduni sanaa na michezo ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Muheza Hamis Mwinjuma (MwanaFA) amepongeza juhudi za Rais Samia katika kuleta maendeleo Wilayani Muheza akisisitiza kuwa miaka minne ya uongozi wake imeleta mafanikio makubwa zaidi ya kipindi cha miaka 46 iliyopita tangu kuanzishwa kwa Wilaya hiyo mwaka 1974.
Aidha MwanaFA amemuomba Rais Dkt Samia kujenga soko la kitaifa la machungwa wilayani humo akitoa sababu kuwa wilaya hiyo ndio mzalishaji mkubwa wa machungwa Nchini.
Naibu Waziri Mwinjuma ameongeza kuwa kumekuwa na changamoto kubwa katika ununuzi wa machungwa wikayani Muheza kwani madalali wengi wamekuwa wakinunua pasipo utaratibu mzuri.
"Mheshimiwa Rais sisi ndio wazalishaji wakubwa wa machungwa kwa miaka yote na wazalishaji wakubwa wa viungo lakini tuna matatizo ya kutokuwa na soko linalofahamika ningeomba kwako mheshimiwa Rais tujengewe soko kubwa la kitaifa la machungwa hapa Muheza kwakuwa sisi ndio wazalishaji wakuu lakini hali kadhalika na soko la kitaifa la mazao ya viungo kwa vile sisi ni wazalishaji wakuu, "alisema MwanaFA.
"Changamoto hii kwenye upande wa machungwa sababu wakulima wanawekeza madalali wanakuja na kununua machungwa yaliyopo mtini kipindi hiki na kununua machungwa yaliyopo mtini kwenye misimu mitatu ijayo ambayo inawasababishia wakulima wetu umasikini mkubwa, "alisisitiza na kuongeza kuwa
"Nina hakika tukipata soko la kitaifa la machungwa hapa kwanza litadhibiti uporomokaji wa bei na kuhakikisha wakulima wetu mazao yao hayaharibiki baada ya kuvuna na kuyatoa kwa bei ya kutupa, "alisisitiza MwanaFA.
Mchana Rais akiweka jiwe la msingi la kiwanda cha saruji
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Stanslaus Nyongo amesema kufuatia maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan, Serikali imefuta tozo 374 ili kuondoa kero kwa wawekezaji.
Mbali na tozo, amesema baadhi ya sheria pia zimefutwa na nyingine kurekebishwa zikiwemo sheria 62, na hivyo kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji.
Nyongo ameyasema hayo leo Februari 27, 2025 wakati wa mwendelezo wa ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan mkoani Tanga, ambapo Rais amefanya ufunguzi rasmi wa mradi wa awamu ya pili ya Kiwanda cha Chokaa na Saruji (Maweni Limestone) kilichopo Jijini Tanga.
Ameongeza kuwa katika mkutano wa Bunge uliopita, imepitishwa sheria ya kuunganisha taasisi mbili za TIC na EPZA zinazowahudumia wawekezaji wa nje na ndani ili kuanzisha mamlaka ya kushughulikia wawekezaji.
Sheria hiyo pia itaruhusu kuanzisha kituo maalumu cha kukaribisha wawekezaji kwa maana ya usajili na kuwatambua kama wawekezaji wa kimkakati.
Vile vile sheria hiyo imelenga kuanzisha Benki ya Ardhi ili wawekezaji wanapokuja Tanzania wakute sehemu ambazo zipo tayari kwa ajili ya uwekezaji.
Akiweka jiwe la msingi wa mradi wa Maji wa Rais ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kushiriki na taasisi nyingine kulinda na kutunza vyanzo vya maji Ili miradi ya maji inayotekelezwa iweze kuwa endelevu
Maelekezo hayo ameyatoa wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika stend ya wilaya ya Mkinga mara baada ya kumaliza uwekaji wa jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Mradi wa Maji Mkinga - Horohoro ambao unatumia chanzo cha Bwawa la Mabayani.
Amesema kuwa Ili mradi huo uweze kuwa endelevu ni muhimu kudhibiti shughuli za kibinadamu kwenye vyanzo vya maji vilivyopo kwenye mkoa huo
"Ujenzi wa Mradi huu unatokana na changamoto kubwa ya maji kuwa na chumvi katika ukanda wa vijiji vya mwambao wa bahari. Hivyo, Mradi huu una lengo la kuboresha huduma ya majisafi na salama kwa wananchi zaidi ya 57,334 wa kata 10 katika vijiji 37 vilivyopo pembezoni mwa barabara ya Tanga -Horohoro pamoja na wananchi wa eneo la Horohoro Mpakani"amesema Rais Samia
Hata hivyo Katibu Mkuu wa Wizara ya maji Mwajuma Waziri amesema kuwa Utekelezaji wa Mradi huu umefikia asilimia 45 ambapo usanifu wa mradi mzima umekamilika na kazi zipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
"Tayari Bomba kubwa za umbali wa km 37 zimeletwa eneo la Mradi, na bomba zenye urefu wa km 25.5 zimelazwa sambamba na Ujenzi wa matanki mawili ya maji yenye mita za ujazo 200 na 250 umekamilika
Pia amesema kuwa Ujenzi wa matanki matatu ya maji yenye mita za ujazo 500 umefikia asilimia 95, naUjenzi wa matanki matano ya maji yenye mita za ujazo 100 umefikia asilimia 90.
Gharama ya mradi wa maji Mkinga-Horohoro unatekelezwa kwa kutumia fedha za Serikali kupitia Mfuko wa Taifa wa Maji (NWF) na utagharimu jumla ya shilingi 35,472,451,838.59 ambapo mpaka sasa fedha zilizolipwa kwa Mkandarasi ni shilingi 11,320,867,775.79.
Kukamilika kwa mradi huu kutasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama wananchi zaidi ya 57,334 waishio katika vijiji 37 vya Wilaya ya Mkinga ambao kwa sasa wanapata huduma ya maji kutoka mbali na maeneo yao na ambayo si salama.
Rais aliwataka wananchi wa Mkinga kumuunga mkono mbunge Dastan Kitandula ambaye ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii kutokana na kazi kubwa anayofanya ya kusaidia serikali katika sekta ya utalii.
"Mbunge wenu msipomuona mjue ananisaodia kazi katika sekta ya utalii mnajua nilikuwa na filamu Ile ya Royal Tour Sasa viongozi wa Wizara akiwemo mbunge wenu wanahangaika kuhakikisha watalii wanakuja nchini kwetu,"alisema Rais.
Rais Leo atakuwa na mkutano mkubwa wa majumuisho katika uwanja wa mkutano ambako atahutumia mamia ya watu wa Tanga akiwa anahitimisha ziara yake.


.jpg)
.jpg)









.jpg)
.jpg)
.jpg)
Comments
Post a Comment