Na. Brigitha Kimario - Bunda
Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) walitembelea eneo la Nyatwali lililopo Wilayani Bunda, Mkoa wa Mara kukagua namna zoezi la uhamaji wa hiari kwa wakazi wa Tamau, Kariakoo, Nyatwali na Serengeti linavyoendelea.
Wakikagua eneo hilo, leo Februari 04, 2025 baada ya kupata taarifa ya maendeleo ya zoezi la Nyatwali kutoka kwa Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Stephano Msumi ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Serengeti, CPA. Hadija Ramadhani alishuhudia majengo mbalimbali yameshabomolewa na asilimia kubwa ya wananchi wa Nyatwali wameshahama na zoezi la ulipaji fidia ya makaburi linaendelea kwa utaratibu mzuri na utulivu.
"Ninawapongeza sana kwa kuendesha zoezi hili kwa mafanikio, mmefanya zoezi kwa weledi na kwa muda mfupi. Tumeshuhudia nyumba zimeshavunjwa na zoezi la uhamishaji makaburi linaendelea bila shaka wengine waje wajifunze kutoka kwenu zoezi kama hili linapojitokeza."
Naye, Dkt. Robert Fyumagwa alisisitiza juu ya ufuatiliaji wa fedha zilizobaki ili zoezi hilo liweze kukamilika.
"Mmefanya kazi nzuri, tumeona ushirikiano wa Wizara, TANAPA, Wilaya hadi Mkoa sasa mjitahidi kufuatilia fedha zilizobaki ili kukamilisha zoezi hili na kama mlivyosema kwenye taarifa wanyama ni wengi wanavuka kwenda Ziwa Victoria hivyo, mjipange namna ya kupunguza wanyama kugongwa".
Akizungumza ofisini kwake, baada ya kupokea ugeni wa wajumbe wa bodi ya wadhamini - TANAPA , Mkuu wa Wilaya ya Bunda Dkt. Vincent N. Anney alisema eneo hili likishakabidhiwa kwa TANAPA ni vyema mnapotangaza vivutio vya Hifadhi ya Taifa Serengeti mtangaze na Ziwa Victoria.
"Ziwa Victoria litangazwe kama bidhaa inayounganisha Hifadhi ya Taifa Serengeti na Hifadhi zingine za maji. Hoteli zijengwe eneo hilo ili watalii waweze kufika upande huu kwa maana wanyama watakuwa wengi na itakuwa fursa kwa wananchi wa Bunda na Mkoa wa Mara kwa ujumla.”
Dkt. Vincent alisisitiza kuwa, ushirikiano uendelee ili zoezi liishe salama, kwa wananchi ambao wameshalipwa fidia zao tuhakikishe wanatoka eneo hilo.
"Tunatarajia mpaka tarehe ishirini mwezi huu zoezi la kulipa fidia ya kuhamisha makaburi liwe limekamilika, wabaki wale wachache ambao fedha zao zitakuja ili kuepuka migongano maana ng'ombe wanachungwa sana. Sasa hatujui ni wa wananchi wanaomalizia kulipwa au la. Alisema Dkt. Vincent
Eneo la Nyatwali linalofahamika kama Ghuba ya Speke lipo Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa Serengeti na lina ukubwa wa ekari 14,250